Mgawanyo wa majimbo Kinondoni wazua mtafaruku - LEKULE

Breaking

24 May 2015

Mgawanyo wa majimbo Kinondoni wazua mtafaruku

Dar es Salaam. Baraza la Madiwani la Manispaa ya Kinondoni limelazimika kupiga kura ili kupitisha mapendekezo ya kuyagawa majimbo ya uchaguzi kutoka matatu ya awali ili yawe matano kama ilivyopendekezwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC).
Dalili za kutofautiana kwa wajumbe hao zilianza kuonekana tangu mwanzo wa kikao baada ya diwani kutoka Chama cha Mapinduzi (CCM) kupendekeza ipigwe kura ya maoni kama wasingekubaliana.

Majimbo yanayotakiwa kugawanywa ni Ubungo, Kawe na Kinondoni.
Kauli hiyo ilipingwa na wajumbe kutoka vyama vya upinzani wakiwamo Mbunge wa Kawe, Halima Mdee na Mbunge wa Ubungo, John Mnyika ambaye aliamua kutoka nje ya ukumbi kwa kile alichoeleza kuwa madiwani wa CCM walishafikia uamuzi kabla ya kuingia ukumbini.
Akizungumza katika kikao hicho, Mkurugenzi wa Manispaa ya Kinondoni, Injinia Mussa Natty aliyataja majimbo mapya kuwa ni Kibamba na Mambwepande na kwamba, uamuzi huo umefikiwa kwa kuangalia kigezo cha idadi ya watu.

“Ukuaji wa miji unawafanya wakazi wengi kuhamia katika maeneo ya pembezoni kwa kasi katika kata za Kibamba, Goba, Bunju, Makubuli, Kimara, Mbweni, Kunduchi na Mbezi ambayo mwaka 2012 yalichukuliwa kuwa ni ya vijijini,” alisema Injinia Natty.
Pia, alisema mapendekezo ya kugawa majimbo hayo yamezingatia mgawanyo wa huduma za kijamii na kiuchumi kama shule, masoko, huduma za afya na miundombinu ya barabara.

Kwa upande wake Mdee alisema NEC imekiuka utaratibu wa kugawa majimbo kwa kuwa Katiba inaitaka tume hiyo kufanya uchunguzi kwanza na kueleza sababu za kugawa majimbo jambo ambalo halijafanyika.
“Siogopi kugawanywa kwa majimbo kwa sababu tunapunguziwa mzigo, lakini nahoji kwanini katika kugawa majimbo baadhi ya kata zimechanganywa? mfano Kata ya Mwananyamala imewekwa Kawe halafu Kata ya Makumbusho ipo Kinondoni?” alihoji Mdee.

Mstahiki Meya wa Kinondoni, Yusuph Mwenda alisema Manispaa ya Kinondoni ina watu milioni 1.8 kwa hiyo kila jimbo sasa litakuwa na takriban watu laki nne.
Baada ya kushindwa kufikia muafaka, Mwenda aliwataka wajumbe kupiga kura, ndipo 10 walinyoosha mikono kupinga uamuzi huo huku 20 wakipendekeza majimbo kugawanywa.
“Walio wengi wameshinda hivyo majimbo yatagawanywa,” alisema Mwenda. Kwa upande wake Mnyika alisema hakubaliani na uamuzi wa kugawanywa kwa majimbo yaliyopo na kuongezwa mengine mawili kwa sababu kufanya hivyo ni kufuja fedha za wananchi.

Akizungumza baada ya kutoka ukumbini, Mnyika alihoji iweje Serikali iliyopinga kuwa na serikali tatu kwenye Katiba Inayopendekezwa ije na mawazo ya kuongeza majimbo mapya 42 nchini nzima.
“Kwenda kama vipofu ni bora kutokwenda kabisa, naiona hatari kwa tume kuja na maamuzi tofauti, mwaka 2010 Kinondoni iliomba kuongezwa majimbo mawili haikupata hata moja, kujadili majimbo matano ni kujilisha upepo,” alisema Mnyika.

No comments: