‘Friends of Lowassa’ kuchangia damu Muhimbili - LEKULE

Breaking

14 May 2015

‘Friends of Lowassa’ kuchangia damu Muhimbili

MAKAMU Mwenyekiti wa marafiki wa Waziri Mkuu wa zamani ambaye pia ni Mbunge wa Monduli, Edward Lowassa, Angel George, amesema mipango imekamilika ya kwenda kuchangia damu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili, jijini Dar es Salaam. 
 
George alitoa taarifa hiyo jana jijini hapa, baada ya kusoma taarifa kwenye vyombo vya habari ikieleza kwamba, Hospitali ya Taifa Muhimbili inakabiliwa na uhaba wa damu. 
 
“Hii taarifa tumeiona, tayari tumewasiliana na marafiki wa Lowassa waitwao Friends of Lowassa nchi nzima na naamini tukimaliza kikao leo, safari ya kwenda kuchangia damu kule Muhimbili ili kuokoa maisha ya Watanzania wenzetu itakuwa tayari.
 
“Kwa hiyo naomba nitumie fursa hii kuwaomba Watanzania wenzetu wanaojali na kuthamini maisha ya Watanzania wote, wajitokeze ili kufanikisha uchangiaji wa damu,” alisema George. 
 
“Sisi ambao ni marafiki wa Lowassa, tumeamua kufanya shughuli hizo za kuisaidia jamii ili kumuunga mkono na kumhamasisha Lowassa anayetarajiwa kutangaza nia hivi karibuni ya kuwania urais kupitia CCM katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba, mwaka huu. 
 
“Hii ndiyo hamasa yetu kwake sisi marafiki zake na tumeamua kuisaidia jamii kwa kuchangia damu ili kuitanguliza jamii mbele. Lakini hata kwake ni hamasa kwamba akifanikiwa kuingia Ikulu, jamii iwe ya kwanza,” alisema.
 
Kupitia vyombo vya habari juzi, Mkuu wa Kitengo cha Mawasiliano na Huduma kwa Wateja cha Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, Aminiel Aligaesha, alisema hospitali hiyo imekumbwa na uhaba wa damu hatua ambayo imelazimu kuomba msaada wa dharura serikalini na kwa watu binafsi. 
 
Alisema uongozi wa hospitali hiyo umewaomba Watanzania, mashirika ya umma, kampuni na watu binafsi, kujitokeza kwa wingi ili kuchangia damu kwa ajili ya kuokoa maisha ya wagonjwa wanaopelekwa hospitalini hapo.
 

“Kwa siku Hospitali ya Taifa ya Muhimbili huhitaji wastani wa chupa za damu 70 hadi 100 na hii inachangiwa na ongezeko la mahitaji ya damu ambayo hutumika zaidi kwa wagonjwa wa dharura, wajawazito, wagonjwa waliofanyiwa upasuaji, watoto na wagonjwa wa saratani,” alisema Aligaesha.

No comments: