Lowassa atajwa tena.....Kada mkongwe atoa ya moyoni juu ya kifungo chake. - LEKULE

Breaking

14 Apr 2015

Lowassa atajwa tena.....Kada mkongwe atoa ya moyoni juu ya kifungo chake.



Wakati Chama Cha Mapinduzi (CCM) kikiendelea kutafakari jinsi kitakavyompata mgombea wake atakayepeperusha bendera ya urais katika uchaguzi mkuu unaotarajia kufanyika mwezi Oktoba mwaka huu, Mwenyekiti mstaafu wa chama hicho mkoa wa Arusha, Yona Merisho Nnko (74), ametoa ya moyoni akisema adhabu iliyotolewa na chama chao kwa makada sita kwa madai ya kuanza mapema kampeni za urais, inamlenga zaidi Waziri Mkuu wa zamani, Edward Lowassa.

Nnko akizungumza na wanahabari nyumbani kwake kijiji cha Kikatiti, wilayani Arumeru, mwishoni mwa wiki iliyopita, alisema makada wote waliopewa adhabu na chama hicho anawafahamu, lakini anayemfahamu zaidi ni Lowassa ambaye pia ni Mbunge wa Monduli kwamba amelegwa zaidi katika adhabu hiyo.

“Lowassa amehisiwa tu kwamba huenda kutokana na uchapaji kazi, uaminifu na uhodari wake wa kuchukua hatua na maamuzi magumu, basi imekuwa nongwa kwa baadhi ya watu wenye chuki ndani ya chama kumzushia mambo bila ushahidi,” alisema.

Alisema wakiwa na Lowassa mwaka 2005 walihangaika sana bila kulala ili kuhakikisha mgombea wa CCM wakati huo, Rais Jakaya Kikwete, anashinda kiti cha urais, na ikawa hivyo.

Alisema hata Rais Kikwete mwenyewe katika nafsi na moyo wake anatambua hilo hata akiamshwa usiku wa manane na kuulizwa.

“Namshauri amuunge mkono ndugu yake lakini asimpendelee,” alisema Nnko ambaye kwa sasa anajishughulisha na kilimo.

Aliwaomba Watanzania wakati ukifika kuhakikisha wanachagua kiongozi atakayejali maslahi yao na ya nchi kwa ujumla.

Alidai kuwa ndani ya chama hicho kwa sasa hakuna anayemfikia Lowassa kwani anajali makundi yote ya wananchi yakiwamo ya vijana, akina mama,wazee na watoto.

“Lowassa amefanya mengi kwa nchi yetu, naomba Watanzania muda ukifika tumchague kuwa Rais wetu na mimi namshauri asiogope muda ukifika achukue fomu agombee kwani wananchi wako nyuma yake,” alieleza.

Hata hivyo, alisema CCM inayo hazina kubwa ya wagombea ambao wanaweza kufaa kwa nafasi yo yote ya uongozi.

Katika hatua nyingine, Nnko alitoa angalizo kuhusu tabia ya kila mmoja ndani ya chama hicho kupayuka na kujifanya ‘msemaji’ wa chama.

Alisema tabia hiyo inakidhoofisha chama huku wanachama wakikosa mweleko, wasijue nani wamsikilize, hali inayotishia kukisambaratisha kabisa chama ikiwa hali hiyo haitadhibitiwa.

Alisema viongozi wa chama wanatakiwa kujenga utamaduni wa kuwa na msemaji mmoja badala ya sasa ambapo kila mmoja amekuwa msemaji jambo ambalo linasababisha chama na wanachama kukosa mwelekeo.

Nnko ambaye alikuwa Mwenyekiti wa CCM, Mkoa wa Arusha kwa kipindi cha miaka 14 mfululizo kuanzia 1993 hadi 2007, alisema vurugu, makundi ndani ya chama pamoja na chuki miongoni mwa baadhi ya viongozi na wanachama yanatishia kukisambaratisha chama hicho.

Alisema kitendo cha baadhi ya viongozi wa juu wa chama hicho kukurupuka na kutoa matamko aliyoyaita ya kupayuka ovyo, huku wakitoa vitisho kwa baadhi ya wanachama bila kufuata vikao halali ni kujitafutia umaarufu na kudhoofisha chama.

Alisema zamani wakati chama kikiwa imara na chenye nidhamu, msemaji wa chama alikuwa mwenyekiti au kama sio yeye basi atatoa kibali maalum kwa katibu mkuu wa chama na matamshi yote ya chama yanatokana na vikao sio kupayuka tu.

Alisema akiwa kama mwenyekiti mstaafu anaamini Rais Kikwete ambaye pia ni Mwenyekiti wa CCM ni kiongozi madhubuti, lakini baadhi ya viongozi wa juu ndani ya chama wanataka wawe maarufu kuliko mwenyekiti kwa kupayuka ovyo nje ya vikao.

Alisema CCM kwa wakati huu kinakabiliwa na upinzani mkubwa hali ambayo inakifanya kuwa dhaifu katika maeneo maeneo mengi hususani ya kuisimamia serikali ili viongozi wake wafuate sheria, kanuni na maadili.

Februari mwaka jana, Kamati Kuu (CC) ya CCM ilitangaza adhabu dhidi ya makada wake sita kwa kuwafungia kugombea nafasi za uongozi ndani ya chama hicho kwa miezi 12, huku pia wakiwa chini ya uangalizi.

Mbali na Lowassa, wengine waliokumbwa na adhabu hiyo baada ya kuitwa na kujojiwa mjini Dodoma ni Waziri Mkuu mstaafu, Frederick Sumaye; Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe; Waziri wa Kilimo, Chakula na Ushirika, Stephen Wasira; Naibu Waziri wa Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia, January Makamba na Mbunge wa Sengerema, William Ngeleja.

Makada hao walipewa adhabu hiyo baada ya kuitwa na Kamati Ndogo ya Nidhamu chini ya Makamu Mwenyekiti wa CCM Tanzania Bara, Philip Mangula, na kuwahoji kwa tuhuma za kuanza kampeni za uchaguzi mkuu ujao kabla ya wakati.

Adhabu dhidi ya makada hao ilimalizika Februari mwaka huu, lakini haijatenguliwa na vikao vya juu vya chama hali inayotia mashaka kuhusiana na hatma yao.

Baadhi yao wamekwishatangaza nia ya kuingia katika kinyang’anyiro cha urais mwaka huu.

Makada wa CCM wanaotajwa kutaka kuwania urais mwaka huu ni pamoja na Lowassa, Sumaye, Membe na Waziri wa Uchukuzi, Samuel Sitta.

Wengine ni Mbunge wa Songea Mjini, Dk. Emmanuel Nchimbi; Ngeleja; Spika wa Bunge, Anne Makinda; Waziri wa Katiba na Sheria, Dk. Asha-Rose Migiro; Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais (Kazi Maalumu), Prof. Mark Mwandosya na Wasira.

Hadi sasa makada wa CCM waliotangaza nia na wanaotajwa kuwania urais kupitia chama hicho ni pamoja na Makamba; Naibu Waziri wa Fedha, Mwigulu Nchemba; Mbunge wa Nzega, Dk. Hamis Kigwangalla; Waziri Mkuu Mizengo Pinda na Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu.

No comments: