TAKUKURU Yabuni Mbinu Mpya ya Kupambana na Rushwa - LEKULE

Breaking

31 Mar 2016

TAKUKURU Yabuni Mbinu Mpya ya Kupambana na Rushwa




Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Mkoa wa Kinondoni imebuni mbinu mpya ya kushirikiana na wananchi kwa urahisi zaidi katika mapambano dhidi ya rushwa kwa kusogeza huduma zake za kiofisi kwa kuwafuata wananchi na kuweka ofisi katika eneo lililowazi ili Wananchi waweze kutoa kero zao na kupatiwa ufumbuzi papo hapo.

Njia hii ya ofisi inayotembea (mobile office) ilizinduliwa rasmi na Mkuu wa TAKUKURU Mkoa wa kinondoni Bw. Benn Lincolin siku ya tarehe 23/03/2016 eneo la Bakhresa Manzese kwa kauli mbiu ‘Mwananchi ulipo TAKUKURU tupo kutatua kero yako ya Rushwa kwa wakati’ inayoenda sambamba na kauli mbiu ya Serikali ya awamu ya tano ya ‘ Hapa Kazi Tu’ kwa lengo la kutoa huduma kwa kuwafuata wananchi mahali walipo na sio kwa kusubiri wao kuleta malalamiko yao katika ofisi za TAKUKURU.

Imeonekana kwamba njia hii itasaidia kutoa elimu kuhusu mapambano dhidi ya rushwa na kurahisisha ufuatiliaji wa fedha za miradi zinazotolewa kwenye Manispaa. Pia itakuwa fursa nzuri ya kuwaelewesha wananchi kuhusiana na sheria katika upatikanaji wa dhamana mahakamani na polisi.

Wito unatolewa kwa wananchi kujitokeza kwa wingi katika maeneo ambayo ofisi hii inayotembea ya TAKUKURU Kinondoni itakapokua ili waweze kupata elimu na kutatuliwa kero zao. Zawadi zitatolewa kwa mwananchi ambae atakua akijibu vizuri maswali ya Chemsha Bongo kwani zoezi hili ni endelevu.

IMETOLEWA NA
MKUU WA TAKUKURU (M) KINONDONI
BENN LINCOLIN
30/03/2016.

No comments: