Muhongo akabidhi gari la wagonjwa la kisasa jimboni kwake - LEKULE

Breaking

5 Mar 2016

Muhongo akabidhi gari la wagonjwa la kisasa jimboni kwake

Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo akifungua mlango wa gari la wagonjwa kabla ya kulikabidhi rasmi.
Daktari Bingwa wa huduma za dharura na Majanga, Dkt. Christopher Mnzava (kulia) akizungumza jambo wakati wa hafla ya kukabidhi gari la wagonjwa la Kituo cha Afya cha Murangi. Kushoto ni Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo
Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo akimkabidhi nyaraka za gari la wagonjwa la Kituo cha Afya cha Murangi, Mganga Mfawidhi wa Kituo hicho, Dkt. Naomi Nyanchara.
Gari la wagonjwa la Kituo cha Afya cha Murangi ambalo limekabidhiwa hivi karibuni. Gari la namna hiyo na la pili nchini na huku lingine lipo Hospitali ya Muhimbili.
Vifaa vya kisasa kwa ajili ya kuhudumia wagonjwa katika gari la wagonjwa la Kituo cha Afya cha Murangi.
Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo akilikagua gari la wagonjwa kabla ya kulikabidhi.


Mbunge wa Musoma Vijijini na Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo amekabidhi gari la kisasa la wagonjwa kwa  Kituo cha Afya cha Murangi, Wilaya ya Musoma Vijijini .

Makabidhiano hayo yamefanyika hivi karibuni kituoni hapo na kushuhudiwa na wananchi mbalimbali kutoka maeneo tofauti ya wilaya hiyo baada ya gari hiyo kukaguliwa kwa kina na Daktari Bingwa wa huduma za dharura na Majanga, Dkt. Christopher Mnzava na kujiridhisha kwamba lipo tayari kwa kuanza kutumika kutoa huduma husika.

Akizungumza kabla ya makabidhiano hayo, Profesa Muhongo alisema gari hilo limetolewa na Serikali ya Japan kwa ajili ya wananchi wa jimbo la Musoma Vijijini lengo likiwa ni kusaidia wananchi hao kuondokana na usumbufu waliokuwa wakiupata.

Alisema kwamba Serikali hiyo ya Japan kupitilia Balozi wake nchini Tanzania, imeahidi kwamba endapo gari hilo litatunzwa na kutumika kwa lengo lililokusudiwa ndani ya kipindi cha miezi sita, wananchi hao wataongezwa gari linguine la aina hiyo.

Profesa Muhongo aliwaagiza wananchi wa jimboni humo kuwa walinzi wa gari hilo ili kuhakikisha linatunzwa vizuri na vilevile linatumika kwa malengo yaliyokusudiwa.

“Ninamuomba Dkt. Mnzava awe anakuja huku mara kwa mara kwa ajili ya kuligakua. Nyie tutakaowakabidhi endapo mtatatizwa na jambo kwenye gari hilo muwasiliane nae ili awapatie maelekezo ya nini cha kufanya.”

Akizungumza wakati wa makabidhiano hayo, Dkt. Mnzava alimpongeza Mbunge huyo kwa juhudi zake za kuhakikisha anamaliza kero mbalimbali zilizokuwa zikiwakabili wananchi wa jimboni humo hususan katika suala la afya.

Alisema kuwa amelikagua gari hilo na kwamba ni gari la kisasa na ni tofauti na magari mengine ya wagonjwa ambayo yapo katika hospitali mbalimbali nchini.

Aliongeza kuwa vifaa vilivyomo ndani ya gari hilo ni adimu na hivyo inapasa watakaokabidhiwa walitunze. “Kwa hapa Tanzania gari la aina hii lipo hospitali ya Muhimbili peke yake; hivyo kwa sasa yapo mawili moja ni hili la Murangi na lingine ni la Muhimbili,” alisema.

Alisema wananchi wa Musoma Vijijini wanayo bahati kubwa kuwa na Mbunge ambaye anajitahidi kushughulikia kero zao kwa kuwatafutia ufumbuzi wa kudumu.

Aidha, kwa upande wa wananchi waliojitokeza kushuhudia makabidhiano hayo, walimpongeza Profesa Muhongo kwa juhudi zake alizozionyesha tangu amechaguliwa za kuwaletea maendeleo.

Nyanjiga Mgeta ambaye alikuwa Kituoni hapo kwa ajili ya kupatiwa matibabu alizungumza na mwandishi wa habari hii na kueleza kuridhishwa kwake na kasi ya maendeleo ya mbunge huyo.

Mgeta alisema hapo awali iliwalazimu wakodi magari ili kufikisha wagonjwa mahututi hospitalini jambo ambalo ni gharama kubwa na vile vile upatikanaji wa magari jimboni humo ni mgumu.

Mwananchi mwingine aliyefahamika kwa jina la Eliza Chilyamkobi alimpongeza Profesa Muhongo na kueleza kwamba gari hilo ni mkombozi kwao na vilevile alimuahidi ushirikiano zaidi na ulinzi wa gari hilo.

Aidha, Profesa Muhongo alisema ifikapo tarehe 6 mwezi huu timu ya madaktari bingwa wapatao sita kutoka China itawasili kituoni hapo kwa ajili ya kutoa huduma ya uchunguzi wa afya na kutoa tiba kwa maradhi mbalimbali.

Alisema madaktari hao vilevile wanakuja na madawa ambayo watayakabidhi kwa wahusika kituoni hapo na huku akiwataka wananchi hao kujitokeza kwa wingi ili kupatiwa tiba bila gharama yoyote.

Katika hafla hiyo, Profesa Muhongo alichangia bati 50 na mifuko ya saruji 234 kwa ajili ya kukamilisha ujenzi wa Wadi ya kina mama na watoto.

No comments: