NAUNDA TUME KUCHUNGUZA SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA WIKI MBILI - LEKULE

Breaking

22 Feb 2016

NAUNDA TUME KUCHUNGUZA SHIRIKA LA ELIMU KIBAHA WIKI MBILI

sim
Waziri wa nchi ofisi ya rais TAMISEMI, utumishi na utawala bora, George Simbachawene wa kwanza kushoto akiwaambia jambo mkuu wa mkoa wa Pwani mhandisi Evarist Ndikilo wa katikati na wa kulia mganga mkuu hospital ya Rufaa ya Tumbi dk. Peter Datan wakati alipotembelea shirika la elimu Kibaha juzi. (Picha na Mwamvua Mwinyi)
Na Mwamvua Mwinyi, Kibaha
Waziri wa nchi ofisi ya rais TAMISEMI, utumishi na utawala bora, George Simbachawene amesema ataunda tume ya watu wachache kutoka wizara hiyo haraka iwezekanavyo ili kuchunguza idara na vitengo vyote katika shirika la elimu Kibaha (KEC) ndani ya wiki mbili. 
Amesema amefikia hatua hiyo baada ya kubaini tatizo kubwa la uongozi hivyo ipo haja ya kuchunguza hali iliyopo kuanzia juu hadi chini.
Aidha Simbachawene alisema tume hiyo itakuwa na kazi ya kupita kila idara na kitengo kuchunguza mambo atakayoyaelekeza kwa siku 14 kisha mwezi march mwaka huu atarejea kufanya ziara na kuzungumza na watumishi.
Alielezea kuwa kuna kila sababu ya kutafakari muundo mzima wa shirika na kuweka mikakati, sheria na mipango ya kisasa na kuondokana na ile iliyopitwa na wakati.
Aliyasema hayo juzi katika ziara yake ya kikazi ya siku moja aliyoifanya shirika la elimu Kibaha ambapo alipata fursa ya kutembelea maeneo ya uwekezaji na shirika kijumla.
Simbachawene alisema katika shirika hilo kuna wachache wanaonufaika na kuneemeka kwa kula hadi wamevimbilwa huku wengine wakiwa wanadidimizwa kimaslahi na kukosa haki zao za msingi.
Alimtaka mwenyekiti wa bodi mpya ya shirika hilo Patrick Makungu na viongozi wengine katika bodi hiyo, kuwa na mawazo mapya ya kuendesha shirika badala ya kufanya kazi kwa mazoea ili kurudisha maendeleo yaliyokuwepo miaka ya nyuma.

Alisema shirika la elimu Kibaha lina miradi mingi, ardhi kubwa na uwekezaji mkubwa hivyo waitumie kujiongezea kipato kwa maslahi ya Taifa na vizazi vijavyo.
Simbachawene alieleza KEC inayumba na kuondoa taswira ya maendeleo na uchumi wake wakati ina vitega uchumi na ardhi kubwa.
“Serikali ya awamu ya tano chini ya rais Magufuli ipo kwa ajili ya kuinua uchumi wa nchi na haitokuwa tayari kuona mashirika ya aina hii yanashushwa hadhi yake na watu wachache na kuwanyima haki watumishi uhuru wa kutembea kiajira na haki zao za msingi “
” Ipo haja ya kuchunguzana na kufanya maamuzi makini kwa kufuata misingi, sheria, kanuni na haki za kiutumishi”alisema Simbachawene.
Hata hivyo alisema uwekezaji wa kampuni ya organia kutoka Egypt iliyowekeza kwenye shirika hilo ni mzuri na wenye tija lakini unaonekana haukuata taratibu na kusababisha maswali kutoka kwa watumishi.
Awali mkurugenzi wa shirika la elimu Kibaha Dk. cyprian Mpemba alisema shirika linakabiliwa na changamoto mbalimbali ikiwemo kupokea wagonjwa wengi 400 hadi 450 kwa siku na madawa.
Dk. Mpemba alitaka serikali kufikisha fedha kwa wakati kwani ni muda mrefu sasa fedha wanazoahidiwa wanatumiwa pungufu tofauti na kiwango wanachoomba hivyo kushindwa kukidhi mahitaji.
Nae mganga mkuu wa hospital ya Rufaa ya Tumbi, dk. Peter Datan alisema kitengo cha maafa hususan ajali (Trauma center) kinakabiliwa na ukosefu wa fedha kwa zaidi ya miaka mitatu sasa.
Katika hatua nyingine waziri huyo alipokea kero mbalimbali kutoka kwa watumishi wa shirika hilo ikiwa ni sanjali na wastaafu shirikani hapo kukosa stahiki zao.
Kero nyingine ni kuondolewa mradi wa kuku ulikuwa ukiingiza bil. 1 na kuingizwa mradi wa mkataba wa Organia ambao hawauelewi maslahi yake, upungufu wa nyuzi, madawa, fedha za allowance na walimu kutopandishwa madaraja kwa miaka sita sasa.
Simbachawene alipokea kero hizo na kuahidi kuzifanyia kazi ambapo kwa upande mwingine aliitaka mganga mkuu dk. Datan kukumbushia fedha walizoahidiwa serikalini ili ombi lao lishughulikiwe haraka.

No comments: