Wahispania Wagundua Tiba ya UKMWI - LEKULE

Breaking

5 Jan 2016

Wahispania Wagundua Tiba ya UKMWI


Wakati dunia ikiwa na zaidi ya watu 34 milioni wanaoishi na Virusi vya Ukimwi (VVU), madaktari nchini Hispania wametangaza kugundua tiba ya ugonjwa huo wanayodai ni uhakika.
Kwa kutumia damu ya kupandikiza kutoka kwenye kitovu mwana (umbilical cord) cha mtu ambaye ana vinasaba ambavyo havipokei virusi hivyo vya Ukimwi, wataalamu hao wa tiba wa Hispania wanaamini kuwa wanaweza kutibu ugonjwa huo baada ya mafanikio waliyopata kwa mgonjwa mmoja.
Madaktari hao wa Kitengo cha Taifa cha Upandikizaji (ONT) cha Hispania walichukua damu ya vitovu mwana vya watu wenye vinasaba ambavyo havipokei VVU na kuipandikiza kwa mtu anayeishi na virusi hivyo. Baada ya miezi mitatu, mgonjwa huyo alipimwa na kuonekana hana virusi.

Daktari wa Programu ya Upandikizaji kutoka Taasisi ya Tiba ya Catalan, Barcelona, Rafael Duarte alisema mgonjwa aliyetibiwa kwa njia hiyo, Timothy Brown (37), alikuwa anaishi na VVU tangu mwaka 2009 na madaktari hao walithibitisha kuwa amepona baada ya kupandikizwa damu hiyo.

Mgonjwa mwingine aliyefanyiwa majaribio ya tiba hiyo alipona VVU, lakini miaka mitatu baadaye alifariki kwa ugonjwa wa saratani.

Timu ya madaktari wa Hispania ililiambia gazeti la kila siku nchini humo la El Mundo kuwa wana uhakika kuwa wameleta mapinduzi katika mapambano ya Ukimwi na magonjwa yanayofanana na hayo.

Dk Duarte alisema mwaka 2015 umekuwa wa kujivunia ugunduzi huo mkubwa duniani, ingawa alitahadharisha kuwa tiba kamili haiwezi kupatikana katika siku za usoni.

Kaimu mkurugenzi wa mwitikio wa Taifa wa Tume ya Kudhibiti Ukimwi Tanzania (Tacaids), Dk Morris Lekule alisema utafiti kama huo hauna budi kufuata taratibu zote na kuthibitishwa na Shirika la Afya Duniani (WHO) kabla ya kutangazwa kuwa ni tiba sahihi.

“Kila mara taarifa zinakuja zikisema tiba ya Ukimwi imepatikana, lakini tiba kupata uthibitisho kwamba ni sahihi, ni mchakato mrefu unaotakiwa kuhakikisha kama kweli dawa hiyo inatibu na ni lazima WHO wathibitishe hilo,” alisema.

Alisema ni vizuri kama wataalamu hao wakapata uhakika kutoka WHO badala ya kuwapa watu matumaini kuwa kuna tiba na baadaye matumaini hayo yanapotea.

Daktari wa kitengo kinachoshughulika na masuala ya Ukimwi cha WHO, Richard Banda alisema hana taarifa za tiba hiyo. Tiba inavyofanya kazi Madaktari wa ONT walitumia damu ya mtu mwenye vinasaba vya ‘CCR5Delta’ ambavyo seli zake haziathiriwi na virusi hivyo vya Ukimwi.

Dk Duarte alisema kwanza huziua seli za damu ya mgonjwa kwa kutumia mionzi halafu seli mpya (kutoka kwenye damu ya mtu mwenye seli zisizoathiriwa na VVU hupandikizwa. Damu hiyo ilipandikizwa kwa mgonjwa mwenye virusi hivyo na saratani ya damu.

Baada ya seli hizo kupandikizwa, Virusi vya Ukimwi vilivyo kwenye damu ya mgonjwa hushindwa kujipenyeza katika seli mpya zilizopandikizwa. “Siku 11 baada ya upandikizaji, mgonjwa wa Barcelona alianza kupata nafuu na baada ya miezi mitatu, tulimpima na kukuta hana VVU,” alisema.

No comments: