TTCL Kurejea Kuwa Mali Ya Umma Kwa Asilimia 100. - LEKULE

Breaking

21 Jan 2016

TTCL Kurejea Kuwa Mali Ya Umma Kwa Asilimia 100.


SERIKALI ipo katika hatua za mwisho za kuilipa kampuni ya Bharti Airtel ili kurejesha umiliki wa asilimia 100 katika Kampuni ya Simu Tanzania, TTCL.

Uamuzi huo unaotarajiwa kutekelezwa kabla ya mwisho wa mwezi huu utaiwezesha TTCL kurejesha hisa zake 35% zilizonunuliwa na Airel mwaka 2001 na kuifanya Bharti Airtel kuwa mbia mwenza katika Kampuni hiyo. 
Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano Prof Makame Mbarawa ametangaza uamuzi huo Jumatatu hii Mkoani Mtwara alipotembelea Ofisi za TTCL Mkoa wa Mtwara, kukagua mitambo na miundo mbinu ya Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano.

"Serikali imesikia kilio cha muda mrefu cha Watanzania na wadau wote wa TTCL kuhusu kuondoka kwa mbia mwenza Kampuni ya Bharti Airtel. Ubia huu wa TTCL na Bharti Airtel utahitimishwa Rasmi kabla ya mwisho wa mwezi huu. 
"Tumefanya majadiliano ya kutosha, tumekubaliana kuwa Serikali iilipe Bharti Airtel sh bilioni 14.9 ili kurejesha hisa za 35% za TTCL na kuifanya Kampuni hii ya TTCL kuwa mali ya Umma kwa 100%.

"Tutatumia fedha za Mapato ya Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano ili kukamilisha utaratibu huu. Naiagiza Bodi na Menejimenti ya TTCL kufanya kazi kwa bidii na Ufanisi Mkubwa na kusimamia kikamilifu shughuki za TTCL ili kutimiza jukumu lake kwa Umma." Alisema Waziri Mbarawa

Kwa upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya TTCL, Prof. Tolly Mbwette amesema, kukamilika kwa mchakato huu ni hatua muhimu sana kwa Uhai na ufanisi wa TTCL na kusisitiza kuwa, mpango wa mageuzi ya kibiashara wa kampuni hiyo sasa utatekelezeka kwa kasi kubwa baada ya hatua hii.

Ofisa Mtendaji Mkuu wa TTCL, Dk. Kamugisha Kazaura amesema, jitihada kubwa za TTCL sasa zitaelekezwa katika kuboresha huduma kwa kutumia fedha za ndani na Mikopo ya wadau wa kibiashara ili kuiwezesha kampuni kuendelea kuwa kiongozi katika utoaji wa huduma bora na nafuu katika soko la Mawasiliano nchini.

Hivi karibuni, TTCL imezindua huduma za Mtandao wenye kasi zaidi wa 4G LTE na kuimarisha ubora wa huduma zake za data na sauti. 

Aidha, TTCL na Benki ya TIB zimeingia makubaliano ya mkopo wa fedha na dhamana za Benki utakaoiwezesha TTCL kupata fedha dola za Marekali milioni 329 ili kuingiza mitambo mipya ya kisasa itakayo boresha huduma zake ikiwa ni pamoja na kuanzisha huduma ya miamala ya fedha kwa njia ya mtandao.

No comments: