Ofisi
ya Bunge inapenda kuwafahamisha Waheshimiwa Wabunge na Wananchi kwa
ujumla kuwa, uteuzi wa wajumbe wa Kamati za Kudumu za Bunge utafanyika
kesho Alhamisi tarehe 21 Januari, 2016, na kufuatiwa na Uchaguzi wa
Wenyeviti na Makamu Wenyeviti wa Kamati husika pamoja na Kamati kupatiwa
maelezo juu ya Wajibu, kazi na Mipaka ya kazi ya Kamati na kupokea na
kujadili Mpango kazi wa Kamati unaoishia Juni, 2016.
Kwa
kuzingatia Kanuni ya 111 ya Kanuni za kudumu za Bunge, Toleo la Aprili,
2013 siku ya Ijumaa tarehe 22 hadi Jumamosi tarehe 23 Januari kutakuwa
na Mkutano wa Wabunge wote ambao pamoja na mambo mengine utakuwa na
lengo la kuwafahamisha Wabunge kuhusu Kanuni za Kudumu za Bunge na
Uendeshaji wa Bunge, Nadharia ya mgawanyo wa Madaraka katika Mihimili ya
Dola, Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge na Mambo Mengine ya Kiserikali.
Aidha,
Kikao cha kwanza cha Kamati ya Uongozi ambacho wajumbe wake ni
Wenyeviti wa Kamati za Kudumu za Bunge chini ya Uenyekiti wa Mhe. Spika,
kinatarajiwa kufanyika Siku ya Jumapili tarehe 24 Januari, 2016, ambapo
Jumatatu tarehe 25 Januari, 2016 itakuwa ni siku mahususi kwa Wabunge
kupata maelezo kuhusu Mpango wa Taifa wa Miaka Mitano unaokusudiwa
kutekelezwa katika Jamhuri ya Muungano.
Ratiba ya Shughuli za Mkutano wa pili wa Bunge unaotarajiwa kuanza Jumanne tarehe 26 Januari, 2016 itatolewa baadae.
Imetolewa na,
Kitengo cha Habari, Elimu na Mawasiliano.
Ofisi ya Bunge,
S.L.P 9133,
DAR ES SALAAM
20 Januari, 2016.
No comments:
Post a Comment