Mwalimu Apigwa Risasi Kichwani Kwa Kosa La Kujisaidia Haja Ndogo - LEKULE

Breaking

18 Jan 2016

Mwalimu Apigwa Risasi Kichwani Kwa Kosa La Kujisaidia Haja Ndogo


POLISI wilayani Igunga mkoani Tabora inamshikilia mfanyabiashara kwa tuhuma za kumjeruhi kwa bastola mwalimu wa Shule ya Msingi Saint Leo.

Akizungumza na waandishi wa habari mwishoni mwa wiki, Kamanda wa Polisi Mkoa wa Tabora, Hamisi Selemani alisema tukio hilo ni la usiku wa Januari 15 mwaka huu katika baa ya Kibo iliyoko barabara ya Mwanzugi mjini Igunga.

Mganga Mfawidhi wa hospitali ya wilaya ya Igunga, Abdallah Ombeni amethibitisha kumpokea Mwalimu Theophano Mvula akiwa na jeraha kichwani ambapo alitibiwa kwa kushonwa nyuzi tatu na kuruhusiwa kwenda nyumbani. 
Kamanda Selemani alimtaja mwalimu aliyepigwa risasi kuwa ni Teophano Mvula mkazi wa mtaa wa Nkokoto kata ya Igunga.

Aidha kamanda huyo alisema chanzo cha kupigwa risasi mwalimu huyo ni kujisaidia haja ndogo jirani na gari la mfanyabiashara huyo, Felix Peter Mselel (42) mkazi wa Nzega.

Alibainisha kuwa baada ya kumuona mwalimu katika gari yake, aliamua kumfuata na baadaye yalitokea mabishano, hali iliyofanya mfanyabiashara kuchomoa bastola na kupiga risasi hewani huku risasi ya pili akimlenga kichwani mwalimu huyo.

Alisema baada ya kupigwa risasi mwalimu alianguka chini ambapo wasamaria walimchukua na kumkimbiza katika hospitali ya wilaya ya Igunga.

Hata hivyo, Kamanda Selemani alisema tayari mshitakiwa amekamatwa pamoja na bastola yake ikiwa na risasi 10 ambapo anategemewa kufikishwa mahakamani wakati wowote ili kujibu tuhuma inayomkabili.

Aidha Kamanda Selemani ametoa mwito kwa kamati zinazojadili na kupitisha majina ya watu wanaoomba kumiliki silaha kuwa makini, kwani bila kufanya hivyo inasababisha kupewa silaha watu wasiokuwa na sifa za kumiliki silaha jambo ambalo ni hatari.


Mwalimu Teophano Mvula akizungumza kutoka hospitali hapo, aliomba serikali kuwa makini na utoaji wa silaha kwa baadhi ya raia.

No comments: