Atiwa Mbaroni Akituhumiwa Kumpa Ujauzito Dada Yake wa Miaka 14 - LEKULE

Breaking

20 Jan 2016

Atiwa Mbaroni Akituhumiwa Kumpa Ujauzito Dada Yake wa Miaka 14



POLISI wilayani Sumbawanga mkoani Rukwa inamshikilia mkazi wa kijiji cha Ulinji, Manispaa ya Sumbawanga mwenye umri wa miaka 28 akituhumiwa kumpatia ujauzito dada yake mwenye umri wa miaka 14 anayesoma darasa la saba.

Inadaiwa kuwa mtuhumiwa ambaye amemtaliki mkewe, alirejea kuishi nyumbani kwa wazazi wake kijijini Ulinji miaka miwili iliyopita kabla ya kumpatia ujauzito mtoto huyo wa baba yake mkubwa.

Polisi imethibitisha kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo juzi saa 8:20 mchana na kufikishwa katika kituo hicho cha Polisi. Alikamatwa na Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Ulinji, Manispaa ya Sumbawanga, Linus Mbutu.

Ofisa Mtendaji wa Kijiji cha Ulinji, Mbutu alisema mtuhumiwa alikamatwa na askari wa Mgambo wa kijiji hicho akiwa amejificha kwa saa tatu porini akikwepa kukamatwa.

“Kukamatwa kwa mtuhumiwa huyo kunatokana na taarifa kutoka kwa walimu ambako msichana huyo alikuwa akisoma baada ya kubainika kuwa ni mjamzito,” alisema Mbutu.

Inadaiwa kuwa wazazi wa msichana huyo wakiongozana na Mwalimu Mkuu wa shule anayosoma pamoja na Ofisa Mtendaji wa kijiji hicho, walitoa taarifa kituo cha Polisi mjini hapa na kupewa hati ya ukamataji yenye namba 297, ambapo walipatiwa fomu ya matibabu (PF.3) kisha msichana huyo akafanyiwa uchunguzi katika Zahanati ya Ulinji .

“Baada ya kufanyiwa uchunguzi wa kitabibu mwanafunzi huyo alibainika kuwa na ujauzito wa miezi minne …alipohojiwa alimtaja mshitakiwa ambaye ni kaka yake akisisitiza kuwa walikuwa na mahusiano ya kimapenzi kwa muda mrefu,” alisema Mbutu.

Baba wa watoto hao (jina limehifadhiwa) alikiri kwamba kijana wake huyo alikuwa ameoa lakini aliachana na mkewe na kurudi nyumbani, ambapo aliendelea kuishi katika familia hiyo bila wao kujua kama watoto wao wana mahusiano ya kimapenzi.

Alisema watoto hao walikuwa wakienda shambani kulima bustani ambako inadaiwa ndiko walikuwa wakikutana na kufanya mapenzi kabla ya walimu kugundua ujauzito wa binti huyo.

Baba huyo alisema mkasa huo umetia aibu kubwa familia yake na wameachia Polisi ichukue hatua kutokana na kushindwa kuvumilia kitendo cha kijana wao ambaye inadaiwa miaka miwili iliyopita, pia alimpa ujauzito dada yake ambaye ni mtoto wa baba yake mkubwa.

Kwa upande wake mama wa watoto hao, alisema huo ni mkosi katika familia yao na hawatawasamehe watoto hao kwa aibu waliyosababishia familia.

No comments: