Dr. Mwaka Amkimbia Naibu Waziri Wa Afya Hamis Kigwangala.........Atakiwa Kujisalimisha Kesho Saa Mbili Wizarani - LEKULE

Breaking

14 Dec 2015

Dr. Mwaka Amkimbia Naibu Waziri Wa Afya Hamis Kigwangala.........Atakiwa Kujisalimisha Kesho Saa Mbili Wizarani


Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Hamis Kigwangala leo majira ya jioni amefanya ziara ya kushtukiza  katika kituo kinachotoa tiba mbadala cha Foreplan Clinic kinachomilikiwa na Dk. Mwaka Juma Mwaka  kilichopo Ilala Bungoni na kujionea hali halisi ya kituo hicho. 
 
Mara baada ya kufika alianza kufanya ukaguzi kuanzia sehemu ya Mapokezi mpaka kwenye vyumba vya matabibu lakini katika vyumba vyote hakuna daktari aliyekuwa anatoa huduma.
 
Akizungumza na wagonjwa waliokuwa wakisubria tiba alisema kuna waliofika katika kituo hicho ili kutibiwa lakini kituo hicho hakina uwezo wa kuwahudumia wagonjwa hao.


Katika ziara hiyo ya kushtukiza ambayo Dr Mwaka na wasaidizi wake walikimbia, msaidizi wa Dk. Mwaka, Bi Teddy L. Mbuya alisema yeye hawezi kusema lolote kuhusu kituo hicho maana yeye sio msemaji mkuu,hivyo alimwomba Naibu waziri kufanya ukaguzi katika kituo hicho pamoja na kuwauliza maswali wahusika mbalimbali wa vitengo vya kituo hicho.
 
Baada ya ukaguzi wa kituo hicho, Naibu Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto, Dkt. Hamis Kigwangala amemwagiza Mkurugenzi Msaidizi Tiba Asilia na mbadala Dk.Paul Mhame ndani ya wiki moja kufanya ukaguzi kwa  kituo cha Dk. Mwaka na aletewe taarifa iliyokamilika kuhusu taaluma ya Dr. Mwaka  pamoja na washirika wake na pia dawa anazozitumia kama ni rafiki kwa wananchi wanaotumia dawa hizo.
 
Pia amesema Dk Mwaka Juma Mwaka amekuwa akijitangaza kupitia vyombo mbalimbali hapa nchini jambo ambalo ni kosa kisheria.
 
Alisema madaktari wana miiko na katika miiko hiyo ambayo inatumika  mojawapo  ni kutojitangaza.
 
 Naibu waziri aliendelea kusema kuwa Dk. Mwaka amekuwa akijiita Dokta na amekuwa akichambua mwili wa binadamu kama vile amesomea udakitari wakati sheria ya tiba asilia na tiba mbadala hairuhusu watu wa tiba Asilia na Tiba Mbadala  kutumia maneno  ya tiba ya kisasa.
 
Pia Naibu Waziri amemtaka Dk. Mwaka Juma Mwaka kufika wizarani kesho saa mbili asubuhi akiwa na nyaraka zake zote zinazohusu utoaji wa huduma ya Tiba Mbadala kwani amekuwa akijiita majina ya tiba za kisasa na pia kutibu kwa njia ya kisasa badala ya kutibu kwa njia ya Asilia au Tabibu.

No comments: