Wabunge Wateule Waitwa Dar Katika Hafla ya Kuapishwa Dk. Magufuli. - LEKULE

Breaking

2 Nov 2015

Wabunge Wateule Waitwa Dar Katika Hafla ya Kuapishwa Dk. Magufuli.


Ofisi Ndogo ya Bunge jijini Dar es Salaam, imewataka wabunge wote wateule walioko majimboni kufika katika ofisi hizo Jumatano wiki hii kwa ajili ya kushiriki hafla ya kuapishwa kwa Rais Mteule itakayofanyika Novemba 5, mwaka huu katika Uwanja wa Uhuru.

Akizungumza na waandishi wa habari jijini Dar es Salaam jana, Kaimu Katibu wa Bunge, John Joel, alisema wabunge wateule watakaohudhuria hafla hiyo wanatakiwa kuja na vyeti vya kuteuliwa walivyopewa na Wasimamizi wa Uchaguzi.

“Kila Mbunge mtarajiwa, atatakiwa kuwasilisha cheti kwa Maofisa wa Bunge wakati wa mchakato wa usajili  na kitambulisho kingine chochote kinachotolewa na mamlaka inayotambulika na kinachomtambulisha jina lake kamili kama linavyoonekana kwenye cheti cha uteuzi wa ubunge,” alisisitiza.

Aidha, alisema mchakato wa usajili wa wabunge wateule utafanyika katika viwanja  vya Bunge la 11 na kuongeza wabunge hao watajitegemea usafiri wa kuelekea bungeni.

Joel alisema mkutano huo utaanza siku ambayo Rais Mteule atakapoitisha Bunge.

Alisema siku hiyo shughuli mbalimbali zitafanyika zikiwamo za uchaguzi na kiapo kwa Spika, viapo vya wabunge, uthibitisho wa jina la Waziri Mkuu, uchaguzi wa Naibu Spika na ufunguzi rasmi wa Bunge la 11.

Alivikumbusha vyama  vya siasa vyenye usajili wa kudumu vinavyotaka kusimamisha mgombea wa nafasi ya Spika vianze mchakato wa kupata mgombea katika ngazi ya vyama baada ya tangazo kutolewa na kuwasilisha jina lake kwa Katibu wa Bunge.

Alivisistiza vyama kuzingatia kuwa mgombea wa nafasi hiyo anaweza kuwa mbunge au mwanachama yeyote wa chama hicho kwa masharti kwamba siyo mbunge mteule.


Hali kadhalika, alisema vyama vya siasa vinatakiwa kuwasilisha jina la mgombea Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec) siku tano kabla ya uchaguzi kujiridhisha kwamba mgombea ana sifa za kuwa mbunge.

No comments: