Lowassa Kuzungumza na Watanzania Kuhusu Uchaguzi Zanzibar na Msimamo wake Baada ya Magufuli Kutangazwa Mshindi - LEKULE

Breaking

15 Nov 2015

Lowassa Kuzungumza na Watanzania Kuhusu Uchaguzi Zanzibar na Msimamo wake Baada ya Magufuli Kutangazwa Mshindi


Aliyekuwa mgombea urais kwa tiketi ya Chadema, Edward Lowassa jana hakuhudhuria mkutano wa kampeni za ubunge mjini Arusha kwa maelezo kuwa anajiandaa kutoa tamko kuhusu hali ya kisiasa visiwani Zanzibar.

Maelfu ya wafuasi wa Chadema jana walifurika kwenye Uwanja wa Ngarenaro mjini Arusha kuhudhuria kampeni za ubunge wa Jimbo la Arusha Mjini ambao uliahirishwa kutokana na kifo cha mgombea kutoka chama cha ACT Wazalendo, lakini wakakumbana na tangazo kuwa Lowassa hataweza kuhutubia na badala yake atakuja siku ya kufunga kampeni hizo.

Mwenyekiti Mwenza wa Ukawa, James Mbatia(NCCR- Mageuzi) naye alisema kuwa Lowassa yupo katika maandalizi ya kikao cha leo kutangaza hatma ya uchaguzi mkuu uliopita.

“Tulikuwa tumepanga Lowassa aje katika mkutano huu, lakini kutokana na kufanya maandalizi muhimu ya mkutano na waandishi wa habari kesho saa 5:00 asubuhi, ameshindwa kuja” alisema James Mbatia, mwenyekiti mwenza wa Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa) unaoundwa na vyama vinne vya Chadema, CUF, NLD na NCCR Mageuzi.

“Lowassa atakuja siku ya kufunga kampeni za ubunge katika Jimbo la Arusha hivyo tunaomba radhi,” alisema Mbatia, ambaye pia ni mbunge mteule wa Jimbo la Vunjo na mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi.

Lowassa, ambaye juzi alikuwa na mazungumzo ya saa moja na nusu na mgombea urais wa Zanzibar, Maalim Seif Sharrif, anatarajiwa kutoa tamko kuhusu hali ya kisiasa visiwani humo ambayo imekuwa tete baada ya Tume ya Uchaguzi (ZEC) kufuta matokeo.

“Mheshimiwa anaandaa mambo muhimu atakayozungumza kesho,” alisema Aboubakar Liongo, msaidizi wa Lowassa alipoulizwa kuhusu waziri huyo mkuu wa zamani jana mchana.

Liongo alisema, mbali na suala la Zanzibar, Lowassa pia ataeleza msimamo wake kuhusu Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25, ambao yeye na chama chake cha Chadema wanaamini kuwa matokeo ya kura za urais yaliyokuwa yanatangazwa na Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) ni tofauti na waliyokuwa nayo.

Tayari Lowassa ameshaeleza kuwa kumalizika kwa uchaguzi wa mwaka huu ni mwanzo wa awamu ya pili ya safari yake ya kuelekea Ikulu, akiwataka wanaomuunga mkono kutokata tama.

“Unaweza kuchelewesha bahati ya mtu, lakini huwezi kuiondoa,” alisema Lowassa, ambaye alishika nafasi ya pili kwa kupata kura milioni 6.07.


Kwenye mkutano wa kampeni mjini Arusha, makamu mwenyekiti wa Chadema-Bara, Profesa Abdalah Safari alisema Lowassa pia atazungumzia tamko la polisi la kuzuia mikutano ya Ukawa na maandamano licha ya kuwa hiyo ni haki yao.

No comments: