Rais Jakaya Atuma Salaam Za Rambi Rambi Kufuatia Kifo Cha Mchungaji Mtikila - LEKULE

Breaking

5 Oct 2015

Rais Jakaya Atuma Salaam Za Rambi Rambi Kufuatia Kifo Cha Mchungaji Mtikila



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ametuma salamu za rambirambi na maombolezo kumlilia Mwenyekiti wa Chama cha Siasa cha Democratic Party (DP), Mchungaji Christopher Mtikila, ambaye alipoteza maisha katika ajali ya gari iliyotokea alfajiri ya  Jumapili, Oktoba 4, 2015, katika Kijiji cha Msolwa, Wilaya ya Bagamoyo, Mkoa wa Pwani.
 
Katika salamu zake za rambirambi kwa Chama cha DP, Rais Kikwete amesema: “ Nimepokea kwa huzuni kubwa taarifa za kifo cha Mwenyekiti wenu na Mtanzania mwenzetu, Mchungaji Christoher Mtikila ambaye nimeambiwa amepoteza maisha katika ajali ya gari Mkoani Pwani akiwa njiani kurejea mjini Dar es Salaam akitokea kwao Njombe.”
 
“Kwa hakika, kifo cha Mchungaji Mtikila ni pigo kubwa kwa Chama cha Democratic Party ambacho kimempoteza kiongozi wake mkuu. Aidha, kifo hicho ni pigo kwa medani za siasa katika Tanzania na kimetunyang’anya mmoja wa viongozi hodari na  wazalendo, aliyekuwa na msimamo thabiti na usioyumba katika kutetea mambo ambayo aliyaamini  katika maisha yake yote,” amesema Rais Kikwete na kuongeza:
 
“Ni jambo la kusikitisha pia kuwa tunampoteza Mchungaji Mtikila katika kipindi cha mchakato muhimu wa kisiasa nchini ambako mchango wake ulikuwa unahitajika sana. Hakika, tutamkosa mwenzetu katika uwanja wa siasa za nchi yetu.”
 
Ameendelea Rais Kikwete, “Nawatumieni nyie wana-democratic Party salamu za dhati ya moyo wangu na pole nyingi kwa kuondokewa na kiongozi wetu mkuu, wa miaka mingi na wenye uzoefu wa uongozi wa chama cha siasa.”
 
“Aidha kupitia kwenu, napenda kuitumia pole zangu nyingi familia ya Mchungaji Mtikila. Nawapa pole sana wanafamilia, ndugu na marafiki na napenda wajue kuwa niko nao katika kipindi hiki cha majonzi ya kuondokewa na mhimili wa familia. Naungana nao katika majonzi. Aidha, naungana nao katika kumwomba Mwenyezi Mungu, Mwingi wa Rehema, aiweke pema roho ya Mchungaji Christopher Mtikila. Amen”.
 
Imetolewa na:
Kurugenzi ya Mawasiliano ya Rais,
Ikulu,
DAR ES SALAAM.
04 Oktoba, 2015