Ananilea Nkya: Magufuli Akichaguliwa Ufisadi Na Umasikini Vitaongezeka - LEKULE

Breaking

6 Oct 2015

Ananilea Nkya: Magufuli Akichaguliwa Ufisadi Na Umasikini Vitaongezeka



Mwandishi wa makala hii ni Ananilea Nkya ambaye ni Mkurugenzi Mstaafu wa TAMWA.
******
Watu wanaokampeni kushawishi Watanzania  wamchague John  Magufuli kuwa Rais wa tano wa Tanzania  kwa kutumia kigezo cha uadilifu wanadhani ataweza  kuzuia  serikali ya CCM kuwa fisadi na hivyo umaskini wa wananchi kupungua.

Kimsingi  wanajidanganya maana  Magufuli akichaguliwa  ufisadi  wa kimfumo unaofanywa na serikali ya CCM ili chama hicho  kibaki madarakani utaendelea kwa kasi na hivyo  pengo kati ya watawala wachache kutajirika kufuru   na mamilioni ya wananchi  maskini wa kutupa litaongezeka mara dufu.

Nchi yetu ilipopata uhuru maadui wa ustawi wa wananchi walikuwa ni watatu—adui mkuu ujinga—  na adui  wengine wawili  wanaotokana na ujinga—adui  umaskini na adui maradhi.

Lakini  katika zama hizi  za utandawazi  na demokrasia ya vyama vingi vya siasa  ameongezeka adui mwingine hatari nchini kwetu–adui  ufisadi.
 
Ufisadi  ameshamiri nchini baada ya mfumo wa vyama vingi vya siasa kuanza mwaka 1992.

Chanzo cha ufisadi  nchini  ni CCM kung’ang’ania madaraka  kwa kutumia nguvu ya fedha  na hivyo serikali yake kila inapochaguliwa   hugeuka kuwa fisadi na kuiba fedha  na mali za umma.

Hivyo, ikitokea  Magufuli akichaguliwa  wananchi wengi wataendelea kuwa maskini  kwa sababu inaelekea  Magufuli mwenyewe au hajui  au haamini kwamba chanzo  cha  umaskini  nchini ni serikali ya  CCM  kuwa fisadi  na kuendekeza rushwa, ubabe, giliba, uongo na siasa za maji taka kushinda uchaguzi.

Inaelekea Magufuli hajatambua  kuwa kuzuia ufisadi unaozaa mafuriko ya wananchi maskini Tanzania kunahitaji  nchi iweke misingi ya kikatiba, lakini CCM kwa  kukataa Katiba Mpya inayotokana na maoni ya wananchi  isiandikwe 2014 iliikataa  misingi hiyo  kwa sababu  kinajua kinanufaika na udhaifu wa kikatiba uliopo sasa.

CCM inachofanya sasa ni Magufuli kuwapumbaza  wananchi kwamba  eti baada ya yeye kuteuliwa kugombea Urais kwa tiketi ya CCM, mafisadi  wameanza kuikimbia CCM.

Magufuli anataka  kuwaaminisha Watanzania kuwa  umaskini  unakabili mamilioni ya Watanzania  umesababishwa na wanaCCM walioondoka kwenye chama hicho baada ya yeye kuteuliwa kugombea Urais!

Pengine ndiyo sababu Magufuli  anaahidi kwenye kampeni zake kwamba akichaguliwa Rais  ataanzisha mahakama ya mafisadi kama alivyokaririwa kwenye mikutano yake ya  kampeni huko Dodoma.

Ninanukuu: ‘’Baadhi ya mafisadi wezi wameanza kukimbia baada ya CCM kuniteua mgombea urais lakini nikiingia Ikulu, nitawafuata huko waliko ili niwashughulikie vizuri ndiyo maana nimesema nitaunda mahakama ya mafisadi’’

Wananchi wanajiuliza kama ufisadi wa fedha  na mali za nchi unafanywa na serikali inayopewa  dhamana ya kuwa mlinzi wa fedha na mali za Watanzania endapo Magufuli atachaguliwa na serikali yake  kuunda mahakama ya mafisadi,  je majaji wa mahakama hiyo  watapata wapi ujasiri wa kumtia hatiani fisadi mkuu  (serikali) wakati kiongozi mkuu wa serikali  (Magufuli) ndiye atakuwa amewateua majaji wa mahakama hiyo?  Je serikali inaweza kujihukumu yenyewe?

Aidha wananchi wanajiuliza   je  serikali  ya CCM imekuwa ikishindwa  kuchukua hatua za kisheria kudhibiti  ufisadi wa  fedha na mali za umma unaofanywa na  serikali ya kwa vile nchi haina  mahakama maalumu ya kushughulikia kesi za ufisadi au ni kwa vile chama chao ni mnufaika wa ufisadi?

Wananchi wanauliza swali hili kwa sababu  ipo  mifano mingi  kuonyesha serikali ya CCM  ni fisadi .

Mfano wa kwanza: Ufisadi wa EPA kuiba kwenye  Akaunti ya EPA benki kuu jumla ya shilingi bilioni 133  mwaka 2005/6.  Wananchi walishangaa kuona Rais wa Jamhuri yetu  alivyopata kigugumizi  kwenye ufisadi huo.
 
Wananchi wanajiuliza  ilikuwaje mlinzi mkuu (serikali ya CCM) kama kweli  haikunufaika na ufisadi wa  EPA haikuchukizwa na kitendo hicho cha aibu na kuchukua hatu za kisheria?

Kadhalika wananchi wanajiuliza, kama kweli wizi huo wa EPA haukuhusisha serikali yenyewe kunufaisha CCM ni kwa nini serikali ya CCM ilisema waliokwapua fedha hizo wamepewa muda wa kuzirejesha benki  na hadi leo (miaka 10 baadaye) haijawatangazia Watanzania  hatma ya fedha hizo?

Mfano wa pili: Ufisadi wa Richmond. Kukotana na ukosefu wa umeme nchini serikali ya CCM iliingia mkataba na kampuni ya kigeni Richmond ili nchi ipate  umeme.

Kabla kampuni hiyo kuanza kuzalisha umeme zilitoka tuhuma kwamba Richmond  ilikuwa ni kampuni feki.

Wakati huo Edward Lowassa  alikuwa Waziri Mkuu,  kimamlaka hakuwa  Waziri wa  Nishati, lakini aliamua kujiuzulu kulinda heshima ya serikali.
 
Lakini cha kushangaza baada ya kujiuzulu Lowassa  kampuni  ya Dowans iliyoirithi Richmond iliendelea kulipwa fedha nyingi kila mwezi hadi zikafikia bilioni 172.

Wananchi wanajiuliza  kama CCM  ilikuwa hainufaiki  na  mabilioni hayo yaliyokuwa yanalipwa  Dowans  na kwamba mnufaika wa ufisadi huo alikuwa ni Lowassa  ni kwa nini Dowans waliendelea kulipwa baada ya Lowassa kuachia ngazi? Ni kwa nini Lowassa hajafikishwa mahakamani hadi leo kama tuhuma dhidi yake zina ushahidi?

Wananchi wanajiuliza  kama CCM na serikali yake wanajinasibu  ni walinzi waaminifu wa  mali na rasilimali za Tanzania na kwamba wanastahili kuendelea kuajiriwa kuwa mlinzi mkuu wa fedha na mali za Tanzania baada ya uchaguzi tarehe 25 Oktoba mwaka huu 2015 ni kwa nini  serikali ya CCM ilipata kigugumizi kumpeleka  Lowassa mahakamani kumdai alipe hizo  shilingi bilioni 172 kama kweli  ndiye aliyenufaika na ufisadi huo?

Mfano wa tatu: Ufisadi  wa  kuuza kwa bei chee  nyumba za Watanzania zenye thamani ya mabilioni ya shilingi huku  leo hii  serikali ikitumia fedha nyingi za umma  kuwapangishia makazi  hotelini  watawala.

Wananchi wanafahamu kuwa  msimamizi  wa   uuzwaji wa nyumba  hizo ulifanyika  wakati  Magufuli akiwa na Waziri nyumba na makazi.

Karibu nyumba za umma elfu kumi ziliondoka mikononi mwa umma na hadi leo Watanzania hawajaelezwa zilipatikana shilingi ngapi kwenye mauzo ya nyumba hizo  na zilitumika kufanya jambo gani la kuwaondolea wananchi umaskini.
 
Aidha katika uuzaji wa nyumba za umma Magufuli anatuhumiwa  kuwauzia baadhi ya ndugu zake.

Wananchi wanajiuliza kama Magufuli na Lowassa wote walikuwa ni watendaji katika serikali ya CCM, na  wote  ufisadi umefanyika  kwenye maeneo ambayo walikuwa na dhamana,  ni kwa nini   leo  Magufuli anashabikiwa na CCM kuwa ni mwadilifu  ili hali  Lowassa akipakaziwa   ufisadi ?

Aidha, wananchi wanauliza  ufisadi   kwa Magufuli katika kusimamia kwa niaba ya serikali ya CCM  uuzaji kwa bei poa nyumba za umma umetoweka  kwa vile tu anagombea Urais kwa tiketi ya CCM na tuhuma za ufisadi kwa Lowassa mkataba wa Richmond umebaki kwa sababu tu ameamua kuondoka CCM na kugombea Urais   kwa tiketi ya CHADEMA –chama kinachowakilisha vyama vinne vya upinzani vinavyoundwa Umoja wa Katiba ya Wananchi-UKAWA?

Mfano wa Nne: Ufisadi wa Tegeta escrow 2014, serikali ya CCM ilifisadi bilioni 306.  Watuhumiwa wa ufisadi huo walienea ofisi mbali mbali za serikali  hadi  ofisi kuu  ya  ya  nchi –Ikulu  inayopaswa kuwa mahali patakatifu ilihusishwa na ufisadi huo!

Tena wananchi walielezwa jinsi mabilioni  ya  fedha hizo zilivyokwapuliwa  kibabe  nyingine zikibebwa  kwa magunia na tandarusi mchana kweupe.

Watawala wa CCM waliopaswa kujiuzulu kama Lowassa alivyojiuzulu  na kisha kupakaziwa ufisadi tuliona jinsi walivyosafishwa  na serikali ya CCM yenyewe!

Wananchi wanajiuliza kama ufisadi wa Richmond haukuwa mkakati wa CCM wa kutumia siasa za maji taka kumtoa Lowassa  kafara wa ufisadi  kudanganya wananchi kwamba  serikali ya CCM siyo fisadi  bali fisadi ni Lowassa ni kwa nini   Magufuli  kwa dhamana yake kama Waziri wa Nyumba  alisimamia ufisadi wa  nyumba za umma  CCM inamuona mwadilifu na Waziri wa nishati  Muhongo  aliyekuwa na dhamana wakati wa ufisadi wa Tegeta escrow alisafishwa ili hali Lowassa   aliyesimamia ufisadi wa  mkataba wa Richmond  anapakaziwa ufisadi?

Zaidi wananchi wanajiuliza kama chanzo cha ufisadi  nchini kama vile Magufuli na CCM wanayotaka kuaminisha umma ni LOwassa na wengine walioondoka CCM,  je  ni kwa nini  serikali ya CCM imekumbwa na ufisadi wa Tegeta escrow  miaka saba baada ya Lowassa kujiuzulu uwaziri mkuu?

Hakika ziko fisadi nyingi  zilizohusisha viongozi wa serikali ya CCM  iwe ni kwenye miradi ya kitaifa au kwenye halmashauri  na  mikataba ya mali za nchi kama vile madini  kuonyesha kwamba  umaskini  wa wananchi unasababisha na  ufisadi wa serikali ya CCM.

Ndiyo  sababu  kwa kutumia mifano hii minne wananchi wanajiuliza  ni kwa nini   CCM imtoe  Edward Lowassa  kafara wa  ufisadi  ili  hali serikali ya CCM ndiyo fisadi?

Kadhalika wananchi  wanajiuliza ni kwa nini Edward Lowassa ambaye ameamua  kuondoka CCM kutumia haki yake ya kikatiba  kutimiza ndoto yake ya kugombea Urais ,  CCM inamuona tishio na hafai kuwa Rais?

Kama alikuwa hafai kuwa Rais  kutokana na ufisadi ilikuwaje alipewa dhamana kubwa  ndani ya serikali ya CCM kuanzia uwaziri hadi Waziri Mkuu na akajiuzulu uwaziri mkuu ili kuzuia serikali ya chama chake isianguke kutokana na ufisadi?

Wananchi wanajiuliza hivi tatizo hapa ni ufisadi wa Lowassa kweli au ni CCM  kutaka kung’ang’ania madaraka ya kuongoza  hata kama wananchi hawakitaki tena chama hicho kiongoze nchi?

Wananchi pia wanajiuliza hivi tatizo ni Lowassa ambaye anao uzoefu mkubwa wa kuongoza serikali na ambaye rekodi yake  inaonyesha kuwa ni mchapa kazi au tatizo ni  kwa vile anagombea   Urais kupitia CHADEM-UKAWA  na  wananchi  wamemkubali ingawa CCM ilidhani umma ungemkataa kutokana na kuchafuliwa kimkakati   kwa  ufisadi?

Wananchi wanajiuliza  kama  Magufuli  ni mwadilifu  kuliko Lowassa na kwamba  CCM  siyo inayonufaika na ufisadi unaofanywa na  watumishi wa serikali yake ni kwa nini CCM wamekataa kuandika Katiba Mpya inayotokana na maoni ya wananchi  ili kuweka misingi ya kikatiba kuziba mianya   kwa  serikali ya chama chochote  kuwa fisadi wa fedha na mali za wananchi?

Wananchi wanajiuliza ni kwa nini CCM  inahaha  kumzuia Lowassa  kuwa Rais  wa Jamhuri  kama CCM  haiogopi   hatari ya kuachia chama kingine kuingia madarakani wakati nchi haijaweka misingi ya kuzuia serikali kuwa fisadi na hivyo wanaogopa kuwa  serikali ya CHADEMA  na UKAWA nayo itakuwa fisadi kama ilivyokuwa serikali ya CCM?

Vile vile wananchi wanajiuliza, kama Rais Jakaya Kikwete ambaye mwaka 2005 alipigiwa kampeni na   CCM  kuwa ni mwadilifu, kama anavyonadiwa  Magufuli sasa  lakini kwa miaka 10 umaskini wa wananchi umeongezeka –deni la taifa  limeongezeka kila Mtanzania  anatakiwa kulipa shilingi 800,000/-—je Magufuli atakuwa na ubavu gani wa kuifanya CCM na serikali yake  isiendelee kuwa fisadi?

Ni kutokana na hoja hizi ndiyo sababu wananchi wengi wanaona kumchagua Magufuli kuwa Rais wa Tanzania ni kuchagua ufisadi na  ni kuchagua mamilioni ya watanzania waendelee na umaskini. HAIKUBALIKI.

Tena  wakati mamilioni ya wananchi wanaendelea kuwa maskini watawala wa serikali ya CCM, familia zao, wapambe wao kwenye kampeni na marafiki zao   wataendelea kujitajirisha kufuru na kwa kujigawia fedha na mali  zinazopaswa kunufaisha Watanzania wote.

Ndiyo sababu wananchi sasa wanahamasishana kutambua kuwa kumchagua Magufuli ni kuichagua CCM na  ni kama  kumpa  tenda  ya ulinzi mlizi mwizi!

Wananchi wanaona ni afadhali kuichagua CHADEMA-UKAWA  kwa sababu kwanza mgombea  wake wa Urais  Lowassa  huenda akaonyesha uadilifu na uchapakazi  wa hali ya juu  kuwathibitishia Watanzania kwamba CCM amepakaziwa na kutolewa kafara ufisadi ili CCM iendelee kubaki madarakani bila kujulikana kwamba serikali yake ndiye malkia wa ufisadi nchini.

Wananchi wanatambua kuwa kuirejesha CCM  Ikulu   kasi ya  umaskini itaongezeka kwa wananchi wengi  kuaendelea kukosa  kipato, kukosa elimu bure na bora hadi chuo kikuu kuondoa adui ujinga na  wizi,  biashara chafu, uvunjifu wa haki za binadamu  na  serikali kuwa mbabe, dikteta mminya demokrasia  vitaongezeka na hivyo kuvuruga amani ya nchi yetu.

Hivyo   ni muhimu serikali ya CCM ikaacha sauti na maamuzi ya wananchi isikike katika uchaguzi mkuu  tarehe 25 Oktoba 2015  ili endapo  wananchi wataamua  kumchagua  Lowassa kama Rais wao kupitia CHADEMA  inayowakilisha vyama vinavyounda   Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA),   waandike Katiba Mpya  inayotokana na maoni ya wananchi na wasipofanya hivyo uchaguzi wa  2010  wananchi wawanyang’anye madaraka.

Katiba mpya siyo tu  itampunguza madaraka ya Rais kuhusu uteuzi wa watendaji ikiwa ni pamoja na majaji wa mahakama, bali pia  itaweka misingi ambayo  mihimili  mitatu ya utawala wa nchi —Serikali, Bunge na Mahakama  vitakuwa haviingiliani.

Kwa hivyo serikali ya chama chochote ikiiingia madarakani na ikafanya ufisadi itawajibishwa na wananchi nao wataacha na wizi na ujambazi wa kutumia silaha kujitajirisha kama watawala wao wanavyoiba fedha za umma kwa kutumia ujambazi wa kalamu.

Katiba Mpya ya wananchi ikiandikwa, serikali ikifisadi fedha na mali za wananchi itashtakiwa  na  majaji hawataogopa  kuihukumu serikali bila  kuipendelea kwa sababu hawatakuwa na woga wa  kupoteza ajira.

Hayo ndiyo mabadiliko wanayotaka wananchi  wa Tanzania katika kukomesha ufisadi wa kimfumo ili kuepusha  ongezeko la wananchi masikini wa kutupa kunakohatarisha amani  na umoja wa  kweli  katika nchi yetu.

Lakini CCM na serikali yake vikitumia rushwa, ubabe na uchakachuaji  katika uchaguzi wa tarehe 25 na  kushinda uchaguzi, tuendako serikali ya CCM itafanya  ufisadi  mkubwa zaidi,  tena ikitumia  ubabe, udikteta na dharau kubwa kwa  vyama vya upinzani na wananchi kwa ujumla.  Mungu ibariki Tanzania.

Note: Ninaruhusu  yeyote anayetaka kutumia , kuchapisha au kusambaza andiko hili afanye hivyo.
------******------------******---------------------*********______

Mwandishi wa makala hii ni Ananilea Nkya ambaye ni Mkurugenzi Mstaafu wa TAMWA.

Anapatikana anapatikana kwa  E-mail:ananilea_nkya@yahoom.co