CCM Zanzibar wazindua rasmi kampeni, Shein aahidi Ushindi wa Kishindo - LEKULE

Breaking

14 Sept 2015

CCM Zanzibar wazindua rasmi kampeni, Shein aahidi Ushindi wa Kishindo


MGOMBEA Urais wa Zanzibar kwa tiketi ya CCM, Dk Ali Mohamed Shein jana alizindua rasmi kampeni zake, akisema hana hofu ya kushindwa na kwamba akirejea madarakani atahakikisha anayalinda kwa nguvu zake zote Mapinduzi ya Zanzibar ya mwaka 1964 huku akiwataka wananchi kulinda amani na utulivu uliopo.

Alisema kinachompa imani ya ushindi ni utekelezaji wa Ilani ya CCM katika miaka mitano ya utawala wake, ambayo kwa kiasi kikubwa imepaisha kasi ya maendeleo Zanzibar. Aidha, amewahakikishia wananchi kuwa Muungano upo imara na ataendelea kuulinda, huku akisisitiza hakuna mtu au kikundi chenye uwezo wa kuuvunja kutokana na misingi ya uanzishwaji wake kuridhiwa na wananchi wa Tanganyika na Zanzibar pamoja na kuwepo kwake kwa mujibu wa Katiba.

Aliyasema hayo kwenye Uwanja wa Demokrasia mjini hapa, wakati wa mkutano wake wa kwanza wa kampeni za Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 25 mwaka huu uliopambwa na viongozi wa kitaifa, wakiwemo marais wastaafu wa Zanzibar na wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakiongozwa na Rais Jakaya Kikwete.

Akizungumza kwa kujiamini, Dk Shein alisema mapinduzi ndiyo yaliyowakomboa wananchi wa Zanzibar kwa hivyo yanatakiwa kulindwa ili yasichezewe na watu wasioyatakia mema. 
 
“Moja ya ahadi yangu mara nilipoingia madarakani ni kuyalinda Mapinduzi ya mwaka 1964 ambayo ndiyo yalimkomboa mwananchi wa Zanzibar,” alisema na kuwataka wananchi kulinda amani iliyopo ambayo imetoa fursa kubwa kwa wananchi kufanya shughuli mbali mbali za maendeleo.

Alisema ilichukua muda mrefu kusaka amani baada ya kutoweka huku akiwataja marais wastaafu, Benjamin Mkapa wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amani Karume wa Zanzibar, kuwa walifanya kazi kubwa kuitafuta.

“Wananchi nawaombeni tuitunze amani iliyopo nchini ambayo viongozi wetu wamefanya kazi kubwa kuitafuta... Amani ikitoweka basi sote tupo mashakani,” alisema Shein. 

Alichukua muda mfupi kuelezea utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya mwaka 2015-2000 ambapo alisema imejikita zaidi katika kuleta maendeleo na ustawi wa wananchi wa Unguja na Pemba.

Aidha, Dk Shein alisema atahakikisha anahubiri amani pamoja na kutekeleza kwa vitendo ahadi zote zilizopo katika ilani ya CCM ili kuwakomboa wananchi na kuondokana na changamoto mbalimbali za kimaisha zinazowakabili.
 
 Dk Shein alisema serikali aliyoiongoza ilihitaji umakini mkubwa sana katika kuiongoza, kitu ambacho aliweza kukitekeleza na kulifikisha taifa hapo lilipo kwa sasa.

“Nilikuwa na changamoto nyingi, lakini sikukurupuka… Sikuwa dhaifu wala mwoga, hivyo waliodhani nilikuwa hivyo wanajidanganya. Sijamwogopa na sitamwogopa yeyote katika utekelezaji wa majukumu yangu zaidi ya Mungu. Atakayeniheshimu nitampa heshima yake…” alisema.

Naye Rais Kikwete alisema wananchi wana kila sababu ya kuichagua CCM ambayo imeleta utulivu mkubwa kwa wananchi wake.
 
Alisema amani iliyopo Zanzibar sasa imetoa fursa kubwa kwa wananchi kufanya kazi zao pamoja na serikali iliyopo madarakani ambayo imekuwa ikiwaletea maendeleo.

Rais Kikwete aliupongeza uongozi wa Dk Shein kwa utulivu na busara kubwa pamoja na hekima katika kuongoza serikali ya Umoja wa Kitaifa yenye mchanganyiko na chama cha upinzani.
 
 “Dk Shein anastahiki kuchaguliwa tena kuwa Rais wa Zanzibar kwa sababu ni kiongozi wa aina yake, mwenye busara na uvumilivu wa hali ya juu licha ya kufanya kazi katika serikali ya umoja wa kitaifa yenye vituko vya upinzani,” alisema.

Kikwete ambaye alitumia fursa hiyo kuwaaga wananchi wa Zanzibar alisema haoni sababu ya Dk Shein kushindwa katika uchaguzi huo kutokana na mambo makubwa aliyoyafanya ikiwemo utekelezaji wa Ilani ya uchaguzi ya 2010-2015.

Alisema anaondoka madarakani huku mambo muhimu yaliyokuwa kero katika Muungano yakipatiwa ufumbuzi wa kudumu ikiwemo suala la mafuta na gesi ambapo alisema sasa hakuna vikwazo ambavyo vitaifanya Zanzibar ishindwe kuchimba rasilimali ya mafuta na gesi.

“Suala la mafuta na gesi tumelipatia ufumbuzi na sasa Zanzibar ruhusa kuchimba na kutafuta rasilimali hiyo na wale waliokuwa wakisema kwamba haiwezekani, basi wamechelewa kwa sasa,” alisema.

Alisema ushindi wa Dk Shein sasa utakifanya Chama cha Wananchi (CUF) kupoteza mwelekeo wa kisiasa Zanzibar pamoja na mgombea wake ambaye atakuwa ameshindwa kwa zaidi ya vipindi vitano.

Mgombea wa CUF ni Maalim Seif Sharif Hamad, Katibu Mkuu wa chama hicho ambaye pia ni Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar ambaye tangu uchaguzi mkuu wa mwaka 1995, amekuwa akishiriki mfululizo, lakini kura zake zikizidiwa na zile za wagombea wa CCM.

“Huyu ndiye Dk Ali Mohamed Shein nawaombeni wananchi mpeni kura za ndiyo ili zimwezeshe kuongoza tena Zanzibar kwa kipindi cha miaka mitano ijayo,” alisema Kikwete na kuongeza kuwa, kwa mafanikio ya utawala wa Dk Shein, hakuna mtu wa kuyabeza kwani kila mtu ameweza kunufaika nayo.

“Wapo wanaosema hakuna maendeleo yoyote yaliyopatikana katika kipindi cha miaka mitano ya uongozi wa Dk Shein wakati hata wao wapo katika serikali hiyo, hao ni waongo na msiwaamini na wapuuzeni. Mkiwapa madaraka wataturudisha nyuma,” alisema Kikwete.

Akizungumzia mafuta, Dk Shein alisema rasilimali hiyo itawanufaisha Wanzanzibari na hadi hivi sasa tayari serikali yake imeshatunga sheria ndogo ambayo inasubiri utekelezaji wake utakaoanza kazi mapema na kuruhusu gesi na mafuta kuanza kuchimbwa visiwani humo.

Dk Shein alisema uchumi wa Zanzibar umekua kwa kipindi cha miaka mitano iliyopita kutoka asilimia 5.2 hadi kufikia asilimia 7.2 kwa kipindi cha sasa. 
 
“Tukianza uchimbaji wa mafuta katika visiwa vyetu uchumi wetu utakua kwa kasi zaidi ya hapa tulipofikia. Nchi itapata kipato kikubwa na maisha ya wananchi wetu yataimarika kwa kila mtu atapata maisha bora,” alisema Dk Shein. 
 
Awali, Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dk Mohammed Gharib Bilal aliwataka Wazanzibari kuendelea kuiamini CCM ambayo imeonesha uwezo mkubwa na mapenzi kwa wananchi wa Tanzania.


Alisema bila ya uongozi wa CCM kushika dola basi Tanzania itayumba kwani upinzani hawana uwezo wa kuongoza nchi. Marais wastaafu wa Tanzania, Ali Hassan Mwinyi na Benjamin Mkapa waliwataka wananchi wa Zanzibar kumchagua tena Dk Shein ambaye ameonesha uwezo mkubwa wa kuwatumikia wananchi wa Zanzibar.

No comments: