Serikali yasifu maandamano ya Lowassa - LEKULE

Breaking

12 Aug 2015

Serikali yasifu maandamano ya Lowassa


Waziri wa Mambo ya Ndani, Mathias Chikawe amesema wamefurahishwa na amani iliyotawala wakati wa maandamano ya kumsindikiza mgombea wa urais wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) Edward Lowassa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) kuchukua fomu juzi.

Waziri Chikawe alisema jana kuwa alishuhudia umati mkubwa wa watu wakiimba na kucheza katika hali ya amani na hilo ni jambo zuri linalopasa kuendelea wakati wote.

Alisema anatarajia hali hiyo itaendelea hata mikoani mgombea huyo akienda.

“Tumefurahi, kulikuwa na amani ya kutosha, watu walikuwa wengi zaidi ya ilivyokuwa kwa CCM,” alisema Waziri Chikawe.

Waziri Chikawe alikiri maandamano hayo kusimamisha shughuli katika baadhi ya maeneo ikiwamo ofisi yake ambayo haikupokea wageni kwa saa kadhaa.

Wakati huohuo, Chikawe alionya: “Tunaomba wanasiasa na mashabiki wao wasitembee na silaha kwenye mikutano yao, waziache mahali salama nyumbani na pia wawaache polisi wafanye kazi yao ya kuwalinda wote.”

Waziri Chikawe alisema mabomu ya machozi yanayotumika kazi yake siyo kuua au kuumiza watu bali kuzuia wasifanye vurugu.

Hata hivyo, Waziri Chikawe alisisistiza ushiriki wa viongozi wa vyama vya siasa ni muhimu katika kufanikisha hilo.

Alisema wanasiasa wanapaswa kujiheshimu kwa kukwepa kampeni za uchochezi na kauli zinazoweza kusababisha fujo.

No comments: