Hulk Aisusia FIFA - LEKULE

Breaking

25 Jul 2015

Hulk Aisusia FIFA

Mshambuliaji kutoka nchini Brazil pamoja na klabu ya Zenit St Petersburg, Givanildo Vieira de Sousa “Hulk” amejiondoa katika orodha ya wanasoka watakaoendesha zoezi la upanjagi wa ratiba na makundi ya kuwania nafasi ya kucheza fainali za kombe la dunia za mwaka 2018.

Hulk, ametajwa kujiondoa katika zoezi hilo litakalofanyika kesho jumamosi, baada ya kuchuikizwa na vitendo vya kibaguzi vinavyoendelea kuonekana katika baadhi ya michezo ya soka nchini Urusi.

Hata hivyo shirikisho la soka duniani FIFA, limetoa taarifa tofauti na madai ya mshambuliaji huyo mwenye umri wa miaka 28, kwa kusema kwamba Hulk amejitoa kutokana na majukumu mengine yanayomkabili.

Hulk amenukuliwa na moja ya chombo cha habari nchini Urusi akisema kwamba amekereka sana na ubaguzi wa rangi alioushuhudia katika baadhi ya michezo ya juma lililopita, hivyo kwenda kwake katika hafla ya upangaji wa ratiba na makundi ni kama kuendelea kubariki vitendo hivyo ambavyo vinatakiwa kukemewa na FIFA.

Hulk alikua kwenye orodha hiyo ambayo imewajumuisha wachezaji wengine kama Ronaldo, Diego Forlan, Fabio Cannavaro, Samuel Eto’o pamoja na Oliver Bierhoff.

Wanasoka hao watakuwa sehemu ya upangaji wa ratiba na makundi ya michezo ya mabara yote duniani, ili kuuwezesha mchakato za kuyasaka mataifa 32 yatakayo papatuana kuwania ubingwa wa dunia mwaka 2018 huko nchini Urusi.




No comments: