Aliyechana Fomu Ya BVR kwa Kukataa Kuvua Hijab Atiwa Mbaroni - LEKULE

Breaking

19 Jul 2015

Aliyechana Fomu Ya BVR kwa Kukataa Kuvua Hijab Atiwa Mbaroni


WATU wawili wamekamatwa katika vituo viwili tofauti vya uandikishwaji wa daftari la mpigakura kwa kosa la kuchana karatasi ya maelezo ya mpiga kura (Fomu namba moja) na mwingine kwa kosa la kujiandikisha mara mbili.

Akizungumza juzi na waandishi wa habari ofisini kwake, Mkurugenzi wa Halmashauri ya Jiji la Arusha, Juma Idd, kuhusu matukio hayo, yaliyotokea Jimbo la Arusha Mjini, alisema Fauzia Abdurai Mussa, ambaye ni binti aliyekuwa amevaa vazi maalumu la hijab alifika kujiandikisha fomu namba moja katika kituo cha YMCA kata ya Kati ambaye alipofika katika eneo la kupiga picha alitakiwa kuvua hijabu ili sura ionekane lakini alikataa.

“Lakini huyu binti alipolazimishwa kuvua vazi hilo alikataa na kutoka nje, na alipofika nje alichana karatasi hiyo ambayo ndiyo fomu namba moja yenye maelezo yake na hapo alikamatwa na askari kutokana na uharibifu wa mali ya serikali na yupo ndani anasubiri kupelekwa mahakamani Jumatatu,” alisema.

Mtuhumiwa wa pili aliyemtaja kuwa ni Daniel Leonard alikamatwa katika kituo cha shule ya msingi Daraja mbili, kata ya Daraja mbili baada ya kudaiwa kujiandikisha Julai 13 na Julai 15, mwaka huu katika kituo hicho, hivyo alitiwa mbaroni.


No comments: