Urais 2015: January Makamba Amwaga Machozi Hadharani - LEKULE

Breaking

26 Jun 2015

Urais 2015: January Makamba Amwaga Machozi Hadharani

Kada wa CCM, January Makamba amejikuta katika wakati mgumu na kumwaga machozi jukwaani alipokuwa akielezea historia ya maisha yake na jinsi walivyoishi  na bibi yake mzaa mama katika kijiji cha Kyaka, wilaya ya Misenyi mkoani Kagera.

Makamba alipanda jukwaani juzi jioni kwa lengo la kuwashuruku wana CCM kwa  kumdhamini,lakini kabla ya hajaanza kufanya hivyo alianza kuelezea maisha yake binafsi na bibi yake wakati huo wakiishi kijijini mwishoni mwa miaka ya 70.

Wakati Makamba akielezea maisha yake yalivyokuwa wakati akiishi na bibi yake, alijikuta sauti ikikwama na kulengwa lengwa na machozi jambo lililomfanya akatishe hotuba na kushuka jukwaani.

Kada huyo ambaye alikuwa mkoani Kagera kusaka wadhamini, baada ya kushuka jukwaani kwa kushindwa kuzungumza alikwenda kwenye kiti alipokuwa amekaa na kukaa kwa muda kabla ya kurudi jukwaani tena kuendelea kutoa shukrani kwa wanachama.

Hata hivyo, baada ya kurudi jukwaani hakutaka tena kuelezea maisha yake na bibi yake walivyokuwa wakiishi, badala yake alianza kuzungumzia changamoto mbalimbali zinazowakabili wananchi wa kijiji cha Kyaka pamoja na mkoa mzima wa Kagera.

Kabla ya kumwaga machozi jukwaani, Makamba aliwaambia wananchi hao kwamba alikaa na bibi yake akiwa anamfundisha kulima, kusalimia watu wakubwa pamoja na kuchunga mbuzi.

Aliwaambia wananchi hao kwamba anayajua maisha ya kijijini kwa kuwa ameishi huko, hivyo  anadhamiria kupambana na ugumu wake ikiwa atapata ridhaa ya CCM kugombea urais kisha kuwa kiongozi wa nchi.

“Nimeishi huku na bibi yangu, najua maisha halisi ya huku na ndiyo maana nasema nataka kuleta majawabu ya changamoto zinazowakabili nyinyi wananchi,” alisema.

Makamba ambaye aliwasili kijijini hapo akitokea Bukoba mjini, alipata mapokezi makubwa ya Pikipiki na magari binafsi ambayo yaliongoza msafara wake hadi ofisi za CCM wilaya ya Misenyi na kupata wadhamini.

Baadhi ya wananchi wa kijiji hicho cha Kyaka walisikika wakiimba nyimbo za Kihaya maalum kwa ajili ya kumkabirisha huku wakisema Makamba amerudi nyumbani.
 
Baada ya kupata wadhamini,  Makamba alipita katika shule ya msingi ya Kyaka ambayo alisoma kuanzia darasa la kwanza hadi la tatu ambako alikutana na mwalimu wake aliyemfundisha darasa la kwanza na kisha alielekea nyumbani kwa bibi yake.

No comments: