Sisitizo la kulindwa usalama na umoja wa Iraq katika kikao cha Marais Rouhani na Fuad - LEKULE

Breaking

14 May 2015

Sisitizo la kulindwa usalama na umoja wa Iraq katika kikao cha Marais Rouhani na Fuad

Akizungumza na waandishi habari katika kikao cha pamoja na rais mwenzake wa Iraq, Rais Dakta Hassan Rouhani wa Iran amesema kuwa usalama wa Iraq ni usalama wa Iran na kusisitiza kuwa Iran iko tayari kuipa nchi hiyo jirani kila msaada inaohitaji kwa ajili ya kulinda uthabiti na usalama wake na vilevile kupambana na magaidi. Katika kikao hicho, Rais Muhammad Fuad Masum wa Iraq ameishukuru Jahmhuri ya Kiislamu ya Iran kwa msaada wake mkubwa kwa nchi hiyo katika mapambano yake dhidi ya magaidi wa Daesh na kuongeza kuwa tokea siku ya kwanza Iran imekuwa ikishirikiana bega kwa began a serikali ya Baghdad katika utumaji silaha kwa Iraq na pia misaada ya kibinadamu kwa ajili ya kuwasaidia wakimbizi wa nchi hiyo. Fuad Masum, ambaye anazuru Iran kwa mara ya kwanza tokea awe rais wa Iraq, aliwasili mjini Tehran Jumanne usiku kwa mwaliko wa Rais Hassan Rouhani. Hata kama viongozi wa nchi mbili hizi jirani wamekuwa wakitembeleana mara kwa mara lakini safari hii ya rais wa Iraq inapewa umuhimu mkubwa katika mazingira nyeti ya hivi sasa kieneo.
Katika miaka ya hivi karibuni nchi za Iraq na Iran zimekuwa zikishuhudia kuimarika kwa ushirikiano wao wa kiuchumi na kibiashara. Mbali na hayo mamilioni ya raia wa nchi mbili hizi jirani wamekuwa wakizuru makaburi na maeneo matakatifu katika pande mbili na hivyo kufanya ushirikiano wa idara na mashirika ya kiutalii ya nchi hizi kuwa jambo la dharura. Hio ndio maana mawaziri wa biashara na utalii wa Iraq wakaandamana na Rais Fuad katika safari yake mjini Tehran. Waziri mwingine muhimu anayeandamana na Rais Fuad katika safari hiyo ni Waziri wa Mazingira wa Iraq. Tatizo la tufani za vumbi na changarawe na vilevile kuenea kwa jangwa ni moja ya changamoto muhimu ambazo katika miaka ya hivi karibuni zimekuwa zikiwasumbua wakaazi wa miji ya Iran inayopakana na Iraq, tatizo ambalo utatuzi wake unahitajia ushirikiano wa karibu wa maafisa wa mazingira wa nchi mbili.
Kuhusu suala la usalama, Iraq inakabiliwa na changamoto kubwa ya hujuma ya magaidi wa Daesh ambao hivi karibuni wameteka mikoa kadhaa muhimu ya nchi hiyo. Hatua za haraka zilizochukuliwa na viongozi wa Iraq kwa lengo la kuisaidia serikali ya Baghdad kupambana na magaidi hao ni suala muhimu ambalo limepelekea viongozi wengi wa Iraq akiwemo Rais Fuad kukiri kwamba Iran ilikuwa nchi ya kwanza kuisadia Iraq kupambana na magaidi waliotajwa. Kwa msingi huo mapambano dhidi ya ugaidi ni miongoni mwa masuala muhimu yanayojadiliwa na viongozi wa Baghdad na Tehran katika mazungumzo yao ya hivi sasa. Katika upande wa siasa, nchi mbili hizi kwa sasa zina misimamo inayofanana kuhusiana na hujuma ya kichokozi ya Saudia Arabia nchini Yemen. Jamhuri ya Kiislamu ya Iran inataka kuwepo kwa usitishaji vita halisi na kufikishiwa misaada ya kibinadamu wananchi wa Yemen ambapo Rais Fuad naye amesema kuwa mzozo wa nchi hiyo hauwezi kutatuliwa kwa njia za kijeshi. Suala jingine linalojadiliwa na viongozi wa nchi hizi jirani ni kuhusiana na udharura wa kulindwa umoja wa ardhi ya Iraq. Siku chache zilizopita kulitolewa ripoti kuwa Congress ya Marekani ina mpango wa kuigawa Iraq katika sehemu tatu za Makurdi, Masuni na Mashia. Baada ya kufanya mazungumzo na rais mwenzake wa Iraq, Rais Hassan Rouhani amesisitiza kuwa nchi hiyo ni moja na iliyo na mshikamano kamili wa kitaifa. Rais Fuad yuko nchini Iran kwa ziara ya siku tatu ambapo atakutana na kuzungumza na viongozi tofauti wa Iran kuhusiana na masuala muhimu ya pande mbili, kieneo na kimataifa.

No comments: