Mramba azungumzia uchumi kwenye msiba wa John Nyerere - LEKULE

Breaking

12 May 2015

Mramba azungumzia uchumi kwenye msiba wa John Nyerere

Dar es Salaam. Aliyekuwa Waziri wa Fedha, Basil Mramba amesema kupungua kwa umaskini kunakoelezwa na baadhi ya wataalamu na wasomi ni suala la kitakwimu ambalo ni gumu kulithibitisha.

Aliyasema hayo jana, Msasani, Dar es Salaam muda mfupi baada ya kuaga mwili wa John Nyerere. Mtoto huyo wa hayati Mwalimu Julius Nyerere, alifariki dunia Mei 9, mwaka huu katika Hospitali ya Taifa Muhimbili na anasafirishwa leo kwenda Butiama kwa maziko.

Alisema ugumu wa maisha umeongezeka na akafafanua kuwa licha ya taarifa zinazotolewa na wataalamu kwamba uchumi umekua ni vyema kila mmoja akajitathmini kuanzia ngazi ya kaya kwani huko ndiko hali halisi iliko.

“Mimi katika kaya yangu bado hatujaendelea. Maendeleo hayajafika kwa kiwango cha kumudu gharama zote kwa kila mmoja wetu. Hatuhitaji kuambiwa juu ya maendeleo yetu kwa kutumia taarifa za kisomi ambazo mara nyingi ni wastani. Angalia familia yako ikoje,” alisema Mramba.

Kauli ya Mramba imekuja siku chache baada ya Benki ya Dunia (WB) kuzindua ripoti yake juu ya maendeleo ya uchumi wa Tanzania, mapema mwezi huu, ambayo inabainisha kuwa katika kipindi kati ya 2007 mpaka 2012, umaskini umepungua kwa asilimia 70 jijini Dar hapa huku ukishuka kwa asilimia 15 mikoani.

Ripoti hiyo pia inaeleza kuwa katika kipindi hicho, umaskini unapungua kwa asilimia moja kila mwaka.
Pia, alielezea kuporomoka kwa shilingi na kubainisha kuwa ni moja ya sababu zinazochangia ugumu wa maisha kwa Watanzania maskini na kueleza kuwa ni jambo linalotaka mikakati makini kukabiliana nalo.

“Dola moja ya Marekani imewahi kuwa sawa na Sh7. Kiasi hicho cha fedha kilikuwa kinaweza kununua mbuzi wakati huo lakini dola hiyo hivi sasa ni Sh2,000. Hebu niambie kiasi hicho kinanunua nini wakati huu?” alihoji Mramba.

Wakati huo huo, familia ya Baba wa Taifa, imelishukuru Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ) kwa msaada ilioutoa katika kipindi chote cha kumuuguza hadi kufariki kwa ndugu yao.
Shukrani hizo zilitolewa na mdogo wa marehemu, Makongoro Nyerere alipokuwa akisoma wasifu wa marehemu mbele ya Makamu wa Rais, Dk Mohammed Gharib Bilal na viongozi wengine waandamizi wa Serikali.

Makongoro alimaliza kusoma wasifu huo kwa taabu kwani alishikwa na majonzi kiasi cha kulia kwa kwikwi na kuwahuzunisha mamia ya waombolezaji msibani hapo.
Aidha, Mbunge wa Monduli, Edward Lowasa ametuma salamu za rambirambi za kumfariji Mama Maria Nyerere na familia ya Baba wa Taifa.

“Nimepokea kwa masikitiko makubwa taarifa za kifo cha John Nyerere, mtoto wa mwasisi wa Taifa letu Mwalimu Julius Nyerere. Kifo chake kimetonesha kidonda siyo kwa familia tu, bali kwa Watanzania wote, kidonda cha kifo cha Mwalimu ambacho bado ni kibichi miaka 16 baada ya kifo chake,” alisema Lowasa

No comments: