Dk Salim, Warioba waonya kuhusu amani - LEKULE

Breaking

20 May 2015

Dk Salim, Warioba waonya kuhusu amani


Dar es Salaam
Mawaziri wakuu wa zamani, Dk Salim Ahmed Salim na Jaji Joseph Warioba wameonya kuwa hali ya mgawanyiko, ubaguzi wa kidini, ukabila na ujimbo miongoni mwa wananchi inatishia umoja na utulivu wa nchi iwapo hatua hazitachukuliwa.
Wakizungumza kwa nyakati tofauti katika mkutano wa siku mbili wa mashauriano kuhusu amani na umoja nchini ulioandaliwa na Taasisi ya Mwalimu Nyerere (MNF) jana, viongozi hao walisema misingi ya amani na utulivu iliyojengwa nchini inastahili kulindwa.
Katika siku za karibuni, viongozi wa dini ya Kikristo na Kiislamu walitofautiana katika ahadi ya Serikali kuingiza Mahakama ya Kadhi kwenye Katiba, suala la Muungano likisababisha mjadala mkali bungeni, huku kukiwa na mapigano ya mara kwa mara ya wafugaji na wakulima.
Dk Salim, ambaye ni mwenyekiti wa bodi ya wadhamini wa MNF, alisema Watanzania wengi wana wasiwasi kuwa amani, umoja na utulivu uliopo hivi sasa nchini unaweza kutoweka iwapo hawatailinda misingi hiyo.
Akifungua mkutano huo uliowakutanisha viongozi wakuu wa Serikali waliopo na wastaafu, viongozi wa dini, wazee na viongozi wa vyama vya siasa, Dk Salim alisema: “Katika kuimarisha amani, umoja na mshikamano Watanzania tuache ubaguzi na kubaguana kwa hisia za kiitikadi, dini, ukabila, mahali mtu anatoka, kazi anayofanya au uwezo wake kiuchumi.
“Na kamwe tusifikiri kuwa amani na umoja ni vitu ambavyo vipo tu… ukiona kuna amani na umoja ujue kuwa zilifanywa jitihada, tena jitihada za kweli kweli.”
Alisema kwa kuwa lengo la vyama vya siasa ni kutawala, haiwezekani kuwa na utawala bora bila kuwa na amani, umoja na mshikamano katika jamii.
 “Tanzania ikipata matatizo hakuna atakayepona. Biashara haiwezekani katika mazingira ambayo nchi haina amani na utulivu; kilimo na ufugaji haviwezekani penye fujo,” alisema Dk Salim ambaye pia amewahi kuwa katibu mkuu wa Umoja wa Nchi Huru za Afrika (OAU).


Jaji Warioba

Akizungumza katika mkutano huo, Jaji Warioba alisema hivi sasa jamii imetawaliwa na udini, ukabila na ukanda na kwamba hata viongozi hawataki kuitwa ‘ndugu’ kama ilivyokuwa enzi za utawala wa Mwalimu Julius Nyerere.
“Maneno kama ndugu yalikuwa yanaleta usawa, leo ukimwita kiongozi ndugu anaona umemdharau,” alisema Jaji Warioba na kuongeza kuwa Serikali ya awamu ya kwanza ilitaifisha shule za dini ili kuleta usawa na umoja lakini hivi sasa hali hiyo imeanza kuondoka.
“Siku hizi ukiniuliza mimi nitakwambia kabila langu fulani, dini yangu ni fulani, natokea ukanda fulani, elimu yangu ni fulani, tumeanza kubaguana,” alisema.
Mkurugenzi mtendaji wa MNF, Joseph Butiku alisema mkutano huo haukusudii kumtafuta mchawi anayetishia kutoweka kwa amani, bali kuzungumza kwa uwazi bila kunyoosheana vidole.
Alisema mazungumzo yatafanyika katika makundi matatu tofauti na wote watajadili viashiria vya kutoweka kwa amani nchini na namna ya kuepukana na hali hiyo.
“Tutajaribu kujibu swali ‘tufanye nini?’. Kikao hakitakuwa na faida kama hatutaweza kujibu swali hilo,” alisema Butiku.
Akitoa salamu kwa niaba ya viongozi wa siasa, mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba alisema hakuna namna Taifa linaweza kuwa na amani kama hakuna haki.
“Ninaamini kikao kitakapomalizika kitatoa mwongozo kwa Taifa kuhakikisha haki inatendeka,” alisema Profesa Lipumba.
Hata hivyo, Profesa Lipumba alisema amesikitika kwa viongozi wa CCM waliopo madarakani kutokuhudhuria katika mkutano huo unaojadili amani.
Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, alisema migogoro iliyopo nchini na mpasuko wa kidini umechangia kuondoka kwa amani na hivi sasa wananchi wengi hawaaminiani.
“Viongozi wa dini hawaaminiani, wazee hawaaminiani, serikalini nao hawaaminiani, wachochezi wanaoondoa amani kwa kiasi kikubwa ni viongozi,” alisema Mbatia. 
Mwenyekiti wa Chama cha Saidia Wazee Tanzania (Sawata), Brigedia Jenerali Francis Mbena alisema ili amani iendelee kuwapo nchini, wazee lazima watumiwe kutoa ushauri.

No comments: