IPTL Kujenga Zahanati Kawe - LEKULE

Breaking

25 Apr 2015

IPTL Kujenga Zahanati Kawe


KAMPUNI ya kufua umeme ya Independent Power Tanzania Limited (IPTL), ambayo ni kampuni tanzu ya Pan Africa Power Solutions (T) Limited (PAP), inatarajia kujenga zahanati katika Kata ya Kawe ili kupunguza tatizo la upatikanaji wa huduma za afya kwa wakazi wanaozunguka kampuni hiyo.

Kauli hiyo imetolewa jana na Katibu na Mshauri Mkuu wa Sheria wa makampuni hiyo, Joseph Makandege, wakati akikabidhi msaada wa vyandarua 700 vyenye thamani ya Sh milioni 10 katika Zahanati ya Wazo na zahanati nyingine zilizopo katika kata za Kunduchi na Kawe.

Alisema msaada huo ambao unalenga kuunga mkono maadhimisho ya siku ya Malaria duniani, umetolewa sasa ili kusaidiana na jamii katika jitihada za kupambana na ugonjwa huo.

“Tumeanza kuchangia katika vita dhidi ya Malaria, na baada ya hapa tunatarajia kuwa na mradi mkubwa wa afya katika kata ya Kawe, tumeanza mazungumzo na viongozi wa kata ya Kawe ili kuona uwezekano wa kujenga zahanati.

“Hii ni moja kati ya maeneo ambayo Mwenyekiti Mtendaji wetu, Harbinder Singh Sethi, na bodi kwa pamoja wameuelekeza uongozi wa IPTL/PAP kujikita zaidi katika awamu hii ya kwanza ya utekelezaji wa mpango mkakati wetu wa uchangiaji katika shughuli za kijamii,” alisema.

Aidha, akizungumza kwa niaba ya Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni, Paul Makonda, Diwani wa Kata ya Wazo, John Moro (CCM), aliipongeza kampuni hiyo kwa kuwajali wananchi katika vita dhidi ya ugonjwa huo.

“Msaada wenu kwa wananchi wa Kinondoni ni kielelezo cha ukaribu wenu kwa jamii ya Watanzania katika kusaidia na kukuza maendeleo nchini. Katika miaka kadhaa sasa Malaria imeendelea kuwa kikwazo kikubwa cha maendeleo ya Taifa kutokana na kusababisha vifo vya nguvu kazi ya Taifa na watoto wachanga ambao kimsingi ndio Taifa la kesho.

“Ninaamini kuwa maafisa wa afya watautumia vizuri msaada huu ili uweze kuwanufaisha akina mama wajawazito wanaokadiriwa kufikia 700, watoto walio chini ya umri wa miaka mitano, wagonjwa wa kutwa na wagonjwa wa kulazwa ili wilaya ya Kinondoni isipoteze nguvu kazi yake kwa ugonjwa huu,” alisema.

Aidha, mmoja wa wakazi wa eneo hilo, Ruth Mahmood, pamoja na kuishukuru kampuni hiyo kuwapatia msaada huo, pia aliiomba serikali iandae makakati wa ujenzi wa jengo la wazazi ambalo litakuwa likitoa huduma zote ili kupunguza adha kwa akina mama wajawazito pindi wanapotaka kujifungua.

No comments: