Mshukiwa wa Al Shabab akamatwa Kenya - LEKULE

Breaking

16 Mar 2015

Mshukiwa wa Al Shabab akamatwa Kenya

Mshukiwa mmoja amekamatwa na polisi kufuatia shambulio la kigaidi lililotokea mjini Mandera kaskazini mwa Kenya siku ya Jumapili usiku, na kusababisha kifo cha mtu mmoja na wengine kadhaa kujeruhiwa.
Idara ya polisi nchini Kenya imesema kuwa mshukiwa huyo alinaswa na maafisa wa polisi na jeshi waliokuwa wakiwasaka washukiwa waliotekeleza shambulio hilo.
Mwandishi wa BBC Robert Kiptoo anasema kuwa Inspekta generali wa polisi nchini Kenya, Joseph Boinet amemdhibitishia kukamatwa kwa mshukiwa huyo, kufuatia shambulizi hilo mjini Mandera.
Akizungumza wakati alipowatembelea maafisa wa polisi na raia waliojeruhiwa kwenye shambulizi lingine lililotokea siku ya Ijumaa mjini Mandera.

Boinet, amesema operesheni inayojumuisha maafia wa jeshi la polisi inaendelea katika sehemu hiyo na kuwa hali ya usalama kwa sasa ni tulivu.
Shambulio hilo lilitokea siku mbili tu baada ya msafara wa gavana wa jimbo hilo kuvamiwa na wanamgambo wa kiislamu kutoka Somalia wa Al shabaab.
Watu watatu waliuawa wakiwemo maafisa wawili wa polisi.
Na katika shambulio la jana ripoti zinasema watu waliokuwa kwenye gari walianza kuwamiminia risasi raia waliokuwa wakinunua vitu katika duka moja, kabla ya kutoweka.
Mmoja wao alifariki papo hapo huku wengine waliojeruhiwa kwa risasi wanaendelea kupokea matibabu katika hospitali moja mjini Mandera.
Kundi hilo la Kiislamu lenya uhusiano na kundi la kigaidi la Al Qaeda limefanya mashambulio kadhaa nchini kenya, tangu wanajeshi wa Kenya walipotumwa nchini humo kuangamiza kundi hilo.
Aidha wamedai kuwa wataendelea mashambulio dhidi ya Kenya hadi kenya itakapoondoa majeshi yake nchini humo.
Lakini serikali ya Kenya imekariri kuwa wanajeshi wake watasalia nchini humo hadi pale kundi hilo litakapotokomezwa kabisa

No comments: