40 watajwa kwa rushwa Sierra Leone - LEKULE

Breaking

18 Feb 2015

40 watajwa kwa rushwa Sierra Leone



Tume ya Kuzuia Rushwa nchini Sierra Leone, ACC imewaamuru watu 40 kufika katika ofisi zake kufuatia ukaguzi wa ndani uliofanyika ambao umetuhumu kwamba mamilioni ya dola ya fedha iliyopangwa kutumika katika kupambana na ugonjwa wa Ebola, haijatolewa maelezo. Imekuja siku chache baada ya ripoti ya ukaguzi kutolewa ikituhumu kuwepo vitendo vya udanganyifu katika kusimamia fedha za nchi kuhusu ugonjwa wa Ebola.
Mwandishi wa BBC kutoka mji mkuu wa Sierra Leone, Freetown, Umaru Fofana amesema ripoti inawajumuisha maafisa wandamizi kutoka wizara ya afya, wafanyabiashara na wanaharakati wa vyama vya kijamii ambao ripoti hiyo imedai kuwa walipokea fedha kwa ajili kutumia katika kampeni dhidi ya ugonjwa wa Ebola.

Mkuu wa ACC, Joseph Kamara ameiambia BBC kuwa watu hao 40 ni sehemu tu ya idadi kubwa ya watu wanaotuhumiwa kwa vitendo vya rushwa nchini Sierra Leone akisema wameanzia chini kupanda juu katika uchunguzi wao.

Amesema kundi lifuatalo litaitwa na ofisi yake mara baada ya watuhumiwa wa sasa kuchunguzwa na kushitakiwa pale unapopatikana ushahidi wa kutosha. Amri hiyo imekuja baada ya chama tawala cha All People's Congress kutoa wito wa kuzuiwa kusafiri nje kwa watu wote waliotajwa katika ripoti hiyo. Katika siku zilizopita watu walioaminika na Tume ya Kuzia Rushwa kuwa na kesi ya kujibu walinyang'anywa hati zao za kusafiria na waliachiliwa kwa dhamana hata kabla ya kesi dhidi yao kuanza rasmi kusikilizwa na mahakama.

Ripoti hiyo imewasilishwa mbele ya bunge la nchi hiyo kujadiliwa.

No comments: