Serikali ya Zanzibar Yasema Uchaguzi wa Marudio Utakuwa Huru na Wa Haki - LEKULE

Breaking

28 Jan 2016

Serikali ya Zanzibar Yasema Uchaguzi wa Marudio Utakuwa Huru na Wa Haki


SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ), imesema imejipanga kuhakikisha Uchaguzi Mkuu wa marudio utakaofanyika Machi 20, mwaka huu unakuwa huru na haki kwa kupambana na makundi ya aina ya watu mbalimbali wanaokusudia kufanya fujo ikiwemo kuwazuia wenye sifa wasipige kura.

Hayo yalisemwa na Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais, Mohamed Aboud wakati alipozungumza na watendaji wa Serikali wakiwemo wakuu wa wilaya na mikoa na baadhi ya vikosi vya ulinzi mjini Chake Chake, Pemba.

Alisema zipo taarifa kwamba kipo kikundi cha watu kimeandaliwa kwa ajili ya kufanya vurugu katika kipindi cha Uchaguzi Mkuu, ikiwemo kuwazuia watu washindwe kwenda kupiga kura kwa malengo ya kisiasa zaidi.

Aboud alisema, Serikali haiwezi kuvumilia watu wa aina hiyo pamoja na vitendo hivyo ambavyo vinakwenda kinyume cha demokrasia ya mfumo wa vyama vingi inayotoa fursa zaidi kwa watu kushiriki katika Uchaguzi Mkuu kwa kuwachagua viongozi wanaowataka.

“Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imejizatiti kuhakikisha kwamba wananchi wote wenye sifa ya kupiga kura katika Uchaguzi Mkuu wa marudio wanatimiza azma ya kidemokrasia ya kupiga kura na vitendo vya kihuni vyenye lengo la kusababisha fujo na vurugu kamwe havina nafasi,” alisema Aboud.

Alifafanua zaidi kuwa chama ambacho hakipo tayari kushiriki katika Uchaguzi Mkuu wa marudio hakina sababu ya kuanza kuweka mikakati ambayo itasababisha watu wengine kushindwa kutekeleza malengo ya kidemokrasia ya kuchagua viongozi wanaotawaka kwa ajili ya kuleta maendeleo.

Alisema, vipo viashiria vya vitendo vya vurugu na fujo vimeanza kujitokeza hivi sasa kwa baadhi ya watu kuandika vikaratasi vyenye muelekeo wa kuleta uchochezi wa kisiasa pamoja na mtizamo wa kuwagawa wananchi wa visiwa viwili vya Unguja na Pemba.

Aboud alisema msimamo wa serikali tayari umetangazwa kupitia Tume ya Uchaguzi ya kufanya uchaguzi wa marudio Machi 20, baada ya ule wa Oktoba 25, mwaka jana kufutwa baada ya kujitokeza kwa kasoro mbalimbali.

Alisema ni wajibu wa vyama vyote vilivyoshiriki katika uchaguzi wa Oktoba 25 kushiriki tena katika mchakato huo ambao ndio halali utakaowafanya wananchi kupata viongozi wao kwa njia ya kidemokrasia ya uchaguzi.

“Msimamo wa Serikali ya Mapinduzi upo wazi kwamba vyama vya siasa vilivyoshiriki katika Uchaguzi Mkuu uliofutwa wa Oktoba mwaka jana vinapaswa kujiandaa na uchaguzi wa marudio,” alisema.

No comments: