13 Nov 2015

Ndugai: Bunge Lijalo ni Balaa



MCHAKATO wa kujaza, kurudisha fomu za kuwania nafasi ya Spikawa Bunge la Jamhuri ya Muungano kwa wagombea ambao si wabunge, umemalizika rasmi jana ambapo mgombea mmoja Profesa Costa Mahalu aliyewahi kuwa 

Balozi wa Tanzania nchini Italia, alishindwa kurudisha.
Wagombea waliorudisha fomu hizo ni Leonce Mulenda, Samuel Sitta, Gosbert Blandes, Dkt. Kalokola Muzzamil, George Nangale, Banda Sanoko, Simon Rubugu na Balozi Philip Marmo.

Wengine ni Dkt. Emmanuel Nchimbi, Julius Pawatila, Dkt. Tulia Ackson, Mwakalila Watson, Dkt. Didas Masaburi, Rita Mlaki, Veroikunda Urio, Chelestino Mofuga, Agnes Makune na Abdullah Ali Mwinyi.

Job Ndugai achukua fomu
Aliyekuwa Naibu Spika katika Bunge lililoisha, Job Ndugai, jana alichukua fomu ya kuwania kiti hicho katika Ofisi ndogo za CCM, iliyopo Lumumba, jijini Dar es Salaam.

Akizungumza baada ya kuchukua fomu, alisema rekodi yake ya kuongoza Bunge inajulikana hivyo hana shaka na uzoefu wa kiti hicho na amewahi kuwa Mwenyekiti wa Kamati za Bunge.

"Sina wasiwasi kuhusu nafasi hii, Watanzania wanajuwa uwezo wangu wa kuwatumikia hivyo naamini wabunge wezangu wateule wakinichagua nitawatumikia kwa uweledi mkubwa," alisema.

Aliongeza kuwa, amepata uzoefu wa kuongoza Bunge kupitia kwa Samuel Sitta, Anne Makinda na akiwa mbunge tangu enzi ya Mzee Pius Msekwa aliyekuwa Mwenyekiti wa Bunge wakati huo.

"Najuwa Bunge la 11 litakuwa na changamoto kubwa, kuna vijana wengi ambao ni wapya lakini naamini nitawatumikia kwa kuwa Bunge linaongozwa na kanuni hivyo nitazitumia kuwaongoza," alisema.

Amzungumzia Samuel Sitta
Ndugai alitumia fursa hiyo kumzungumzia Mzee Sitta akisema anatambua kuwa ni mwalimu wake lakini mwalimu hawezi kumzidi mwanafunzi hivyo hana shaka naye bali anaamini atachaguliwa.

Rita Mlaki 'afunguka'
Akizungumza mbele ya wandishi wa habari, Mlaki alisema amekaa bungeni miaka 10 kama mbunge na ameshika nafasi mbalimbali hivyo amepata uzoefu wa kutosha na anaweza kuitumikia nafasi hiyo.

"Nataka nafasi hii ili niweze kushirikiana na wabunge wenzangu kupitisha Miswaada muhimu yenye maslahi kwa wananchi na kuweza kuisimamia," alisema.

Aliongeza kuwa, lengo lingine la kuwania nafasi hiyo ni kuhakikisha anasimamia suala zima la bajeti ya nchi na kuisukuma Serikali iweze kukusanya mapato yake ya ndani bila kuwategemea wahisani.

Akizungumzia nafasi ya mwanamke, alisema Bunge lililopita lilikuwa na Spika mwanamke hivyo si tatizo kama ataingia tena mwanamke kutokana na uwezo walionao sawa na wanaume.

Balozi Marmo arudisha fomu
Katika hatua nyingine, mgombea wa nafasi hiyo Balozi Philip Marmo, jana alirudisha fomu wa kuwania nafasi hiyo na kujivunia rekodi yake ya utumishi akidai ana uzoefu uliotukuka.

Alisema amesukumwa kugombea nafasi hiyo baada ya Rais Dkt. John Magufuli kushinda nafasi ya urais katika Uchaguzi Mkuu uliofanyika Oktoba 25, mwaka huu, kwani ni mtendaji mzuri ambaye anaamini atafanyakazi ya kuijenga nchi ipige hatua ya maendeleo.

"Najua Bunge la sasa litakuwa la kisasa kutokana kwa sbabu limejaa vijana wengi lakini nawaahidi, nitaliongoza Bunge hilo kisasa zaidi na kuwafanya wabunge watekeleze wajibu wao ipasavyo," alisema.

Dkt. Didas Masaburi naye arudisha fomu
Mgombea mwingine wa nafasi hiyo aliyerudisha fomu jana ni aliyekuwa mgombea ubunge Jimbo la Ubungo, Dkt. Masaburi na kusema anafiti kuwa Spika kwani ana ubora unaozidi wagombea wote wa nafasi hiyo.

Alisema ana uzoefu wa kutosha kwani amewahi kuwa Mbunge wa Jumuiya ya Afrika Mashariki hivyo atahakikisha Bunge linaisimamia Serikali katika mikataba mbalimbali kwa maslahi ya nchi.

Mchakato wa kuchukua na kurudisha fomu kwa wagombea ambao ni wabunge wateule unaisha Novemba 14, mwaka huu.

No comments:

Post a Comment