14 Oct 2015

RAIS KIKWETE KUWEKA JIWE LA MSINGI LA UJENZI WA BANDARI YA BAGAMOYO

RAIS KIKWETE KUWEKA JIWE LA MSINGI LA UJENZI WA BANDARI YA BAGAMOYO


Na Mwandishi Wetu
 RAIS Jakaya Kikwete Alhamis Wiki hii anatarajiwa  kuweka jiwe la msingi la ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo mkoani Pwani.  

Mradi huo wa ujenzi wa bandari ya Bagamoyo utakaokuwa wa aina yake Afrika Mashariki na Kati, unatarajiwa kugharimu dola za Marekani bilioni 10.

Kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa kwa vyombo vya habari na Katibu Mkuu, Ofisi ya Waziri Mkuu Dk Florens Turuka, Rais Kikwete ataweka jiwe hilo la msingi kwa ajili ya uzinduzi wa awamu ya kwanza ya mradi; ambayo ni ujenzi wa wa bandari hiyo iliyopo wilayani Bagamoyo.

Turuka alisema, mradi mzima wa ujenzi utajumuisha eneo hekta 800 kwa ajili ya ujenzi wa bandari na eneo la hekta 1,700 kwa ajili ya ukanda wa viwanda.

Eneo hilo  litaendelezwa chini ya makubaliano ya Serikali ya Tanzania, Kampuni ya China ya Merchants Holdings International (CMHI) na Mfuko wa Taifa wa Dharura wa Oman (SGRF).

Chini ya ushirikiano huo, Serikali inawakilishwa na Mamlaka ya Bandari ya Tanzania (TPA) na Mamlaka ya Maeneo Maalum ya Uwekezaji kwa Mauzo ya Nje,(EPZA), Oman itawakilishwa na SGRF na China CMHI.

“Pamoja na bandari na ukanda wa viwanda, mradi huu pia utahusisha ujenzi wa miundombinu kama vile reli, mitandao ya barabara, umeme, umeme, gesi na mitandao ya mawasiliano,” alisema Dk Turuka.

Mradi huo unatarajiwa kuibadili Tanzania na kuwa kituo kikuu cha usafirishaji kwa wafanyabiashara wa ndani na wa kimataifa ambao wataunganishwa na viwanda vitakavyozalisha bidhaa zilizoongezewa ubora.
Kwa mujibu wa Dk Turuka, wazo la kuwepo mradi huo, limetokana na uhusiano wa muda mrefu wa kidiplomasia baina ya Tanzania, China na Oman katika kuhamasisha uimarishaji wa viwanda Afrika jambo litakalosaidia kuongeza ajira nchini.

Kuanzishwa kwa mradi huo, kuliibuka tangu mwaka 2008, Rais Jakaya Kikwete alipotembelea China na kuzungumza na Rais wa nchi hiyo, Hu Jintao, na kuafikiana kujenga bandari hiyo.

Sherehe za kuweka jiwe la msingi zitahudhuriwa na wageni wa kimataifa na wa ndani wakiwemo wawekezaji katika mradi huo.
Wengine wanoatarajiwa kuhudhuria ni, wana diplomasia na ujumbe kutoka kwa Sultani wa Oman utakaoongozwa na Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano nchini humo, Shehe Abdullah Al Saadi.

Ujumbe kutoka China utaongozwa na Mkurugenzi Mtendaji wa CMHI ambaye pia ni Makamu wa Rais Mtendaji wa kampuni ya China Merchant Group Dk Hu Jianhua.

No comments:

Post a Comment