Mwenyekiti
wa Taifa wa Chama cha NCCR-Mageuzi, James Mbatia amepita bila kupingwa
katika mchakato wa kumtafuta mgombea ubunge jimbo la Vunjo, mkoani
Kilimanjaro kupitia chama hicho.
Mbatia
amepitishwa baada ya vikao vya Kamati ndogo kwenye ngazi ya matawi,
kata na jimbo kumpa alama ‘A’ sawa asilimia 100 baada ya kuwa mgombea
pekee aliyejitokeza kuomba kuteuliwa na chama chake kuwania ubunge.
Katibu
wa NCCR Mageuzi jimbo la Vunjo, Mathew Temu alisema Mbatia alipitishwa
na vikao hivyo wiki iliyopita hasa kutokana na mchango wake katika
chama, uwezo na nia ya kulikomboa jimbo kutoka mikononi mwa Chama cha
Tanzania Labour Party (TLP).
Alisema Mbatia alichukua fomu na kuirejesha Juni 29, mwaka huu.
“Waliompitisha
ni wajumbe wa kikao halali cha jimbo la Vunjo; kwa kuwa mchakato huo
ulianzia kwenye ngazi za matawi na Kata,”alisema Temu.
Naye
Mjumbe wa Halmashauri Kuu ya Taifa ya NCCR-Mageuzi, Hemed Msabaha
alisema kamati ndogo zilipewa mamlaka ya kufanya uteuzi kwa niaba ya
Halmashauri Kuu na hivyo jina la Mbatia lilishapitishwa rasmi.
Mbatia
anakuwa kiongozi wa pili mwandamizi wa vyama vinavyounda Umoja wa
Katiba ya Wananchi (Ukawa), kupita bila kupigwa katika mchakato wa kura
ya maoni ya kiti cha ubunge baada ya juzi wajumbe wa Mkutano Mkuu Maalum
wa Uchaguzi Wilaya ya Hai, kumchagua Mwenyekiti wa Chama cha Demokrasia
na Maendeleo (Chadema), Freeman Mbowe kwa kura 269.
Mbowe
naye alipita bila kupingwa katika mchakato wa kura ya maoni ya ubunge
wa jimbo la Hai, baada ya kuvuna kura 269 sawa na asilimia 98.2.
Wakati
huo huo, Mkutano Mkuu Maalum Wilaya ya Mwanga, ulimchagua Hendry Kilewo
kwa kura 109, kuwa mgombea wake wa kiti cha ubunge.
Kada
huyo aliwashinda Mdimu Ngoma aliyepata kura 25, Joyce Mfinanga kura 38,
Mengi Kigombe kura 2 na Nurdin Jela aliyeambulia kura moja.
No comments:
Post a Comment