Wabunge Wataka Wanaoharibu Miundombinu ya DART wachukuliwe hatua Kali - LEKULE

Breaking

1 Apr 2016

Wabunge Wataka Wanaoharibu Miundombinu ya DART wachukuliwe hatua Kali


KAMATI ya Bunge ya Utawala na Serikali za Mitaa imeiagiza serikali kuwachukulia hatua kali wale wote waliovamia miundombinu ya Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka (BRT) na kuigeuza kuwa masoko ya bidhaa zao.

Mwenyekiti wa kamati hiyo, Jasson Rweikiza amesema hali hiyo haivumiliki na inapaswa kukomeshwa mara moja.

Kamati hiyo ilikutana kwa mara ya pili na uongozi wa Wakala wa Mradi wa Mabasi Yaendayo Haraka (DART) jana jijini Dar es Salaam.

“Tumejionea katika ziara yetu tuliyoifanya katika miundombinu ya mradi kuwa baadhi ya wafanyabiashara wadogo wameivamia miundombinu na kuigeuza kuwa masoko,” alisema.

Rweikiza ambaye pia ni Mbunge wa Bukoba Vijijini alisema jambo hilo haliwezi kufumbiwa macho kwani mradi huo umegharimu fedha nyingi na zitalipwa na kodi ya Watanzania.

Alisema pia baadhi ya madereva wa magari na pikipiki maarufu kama bodaboda wameharibu baadhi ya miundombinu na kwamba wanatakiwa kudhibitiwa.

Aliitaka serikali kuweka ulinzi na wote wanaobainika wachukuliwe hatua kali za kisheria.

Aliutaka uongozi wa DART kuipatia majibu kamati yake kulingana na maswali waliyouliza ifikapo Aprili 4 mwaka huu.

Kamati ilitaka kujua miongoni mwa mambo mengine suala la nauli za mabasi, tarehe ya kuanza kwa mradi, na mkataba kati ya DART na mtoa huduma wa mpito wa mradi.

Kaimu Mtendaji Mkuu wa DART, Ronald Lwakatare alisema wakala umejipanga kutoa majibu kwa kamati ya Bunge kwa wakati ili kuiwezesha kuzifahamu kazi za wakala na changamoto zilizopo.

 “Tunazo changamoto nyingi zikiwemo za ofisi, uchache wa wafanyakazi, ufinyu wa bajeti na uharibifu wa miundombinu,” alisema.

Alisema kamati hiyo, serikali na wakala zinatakiwa kuwa karibu ili awamu ya kwanza ya mradi iweze kukamilika na kuanza na awamu nyingine.

Naibu Waziri, Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (Tamisemi), Suleiman Jaffo aliwataka wananchi kuendelea kuwa na subira na kuahidi kuwa mradi huo utaanza hivi karibuni na kutoa huduma nzuri ya usafiri.


“Kuna mambo yanakamilishwa ndani ya serikali na wadau wake yakiwemo kufunga mfumo wa utozaji nauli kwa njia ya kadi na mengine,” alisema waziri huyo ambaye pia ni Mbunge wa Kisarawe. 

Alisema nauli zitakazotozwa katika mradi huo zitakuwa rafiki kwa wananchi hivyo wasiwe na wasiwasi.

No comments: