Kutoka Bungeni: Serikali Kujenga Vyuo Vya VETA kila Wilaya - LEKULE

Breaking

1 Feb 2016

Kutoka Bungeni: Serikali Kujenga Vyuo Vya VETA kila Wilaya

Serikali kupitia Wizara ya Elimu,Sayansi,Teknolojia na Ufundi  inatarajia kujenga Vyuo vya Ufundi (VETA) kwa kila wilaya ili kutoa fursa kwa wananchi wengi hususani vijana kupata mafunzo mbalimbali ya ufundi  yatakayowasaidia kujikwamua kiuchumi na kujenga taifa.

Hayo yamesemwa leo Bungeni na Naibu Waziri wa Elimu,Sayansi,Teknolojia na Ufundi  Mhe. Mhandisi Stella Manyanya  wakati akijibu swali la Mbunge wa Lupa Mhe.Victor Kilasike Mwambalaswa (CCM) kuhusu ujenzi wa vyuo vya VETA  kwa kila Wilaya ambapo Wilaya ya Chunya ni moja kati ya Wilaya kumi za mwanzo zilizo katika mpango wa ujenzi wa vyuo hivyo .

Naibu Waziri huyo amesema Serikali kwa kutambua umuhimu wa kuwa na Chuo hicho  Cha VETA , tayari maandalizi ya awali ya ujenzi wa chuo hicho ikiwa ni pamoja na kufanya utambuzi wa stadi zinazohitajika  yamekamilika.

“Natoa wito kwa wabunge katika majimbo yao kwa kushirikiana na Halmashauri za Wilaya zote watafute ardhi kwa kutenga maeneo maalum kwa ajili ya ujenzi wa vyuo hivi ili hata mipango ya ujenzi ikikamilka ikute eneo lipo tayari kwa kuanza utekelezaji wake”Alisema  Mhe.Manyanya.

Mhe. Mhandisi Stella Manyanya amesema katika mwaka wa fedha wa 2015/2016 Wizara hiyo kupitia Mamlaka ya Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imeshateua wataalamu elekezi watakaoshindanishwa kutayarisha andiko la jinsi ya kuifanya kazi ya kubuni majengo na kupata gharama ya kazi hiyo ili kuanza ujenzi mara moja.


Serikali kupitia Wizara ya Elimu,Sayansi,Teknolojia na Ufundi  kwa kushirikiana na Mamlaka ya Mafunzo ya Ufundi Stadi (VETA) imejipanga kutoa elimu bora ya ufundi yenye kuleta ufanisi katika maendeleo ya ufundi stadi nchini ili kuwawezesha  wahitimu kupata ujuzi ulio bora kwa maendeleo yao na taifa kwa ujumla.

No comments: