Shirikisho la Wamiliki wa Shule Binafsi Waipongeza Serikali Kwa Kufuta Mfumo wa GPA na Kurudisha Division - LEKULE

Breaking

21 Jan 2016

Shirikisho la Wamiliki wa Shule Binafsi Waipongeza Serikali Kwa Kufuta Mfumo wa GPA na Kurudisha Division


Shirikisho la wamiliki wa shule na vyuo visivyo vya serikali  TAMONGSO watoa pongezi kwa Serikali kupitia Wizara ya Elimu, Sayansi Teknolojia na Ufundi kwa kuliagiza Baraza la Taifa la Mitihani kufuta mfumo unaotumika sasa wa Wastani wa Alama (GPA) na kurudi katika mfumo uliokuwa unatumika hapo awali wa division.

Akizungumza na waandishi wa habari leo jijini Dar es salaam Mwenyekiti Taifa wa TAMONGSO Bwa. Mrinde Mzava amesema kuwa Waziri wa Elimu Ameitendea haki Sekta ya Elimu kwani mfumo huo ulileta sintofahamu kwa wananchi wengi.

“Waziri ameitendea haki sekta ya Elimu kwani mfumo wa GPA ulileta sintofahamu kwa wananchi na pia ulikuwa unaongeza ufaulu usio na mashiko kwa wanafunzi walio wengi ukilinganisha na mfumo uliokuwa unatumika awali,” aliongeza Mwenyekiti huyo.

Vilevile Mwenyekiti huyo alisema kuwa Tanzania inahitaji kuingia kwenye soko la upinzani hasa katika sekta ya Elimu  ili iweze kuajiri watu wenye utaalamu na sifa stahiki na kuweza kushindanishwa kwenye soko la kimataifa hivyo kwa mfumo wa GPA ulikuwa unadidimiza elimu ya Tanzania.

Mbali na hayo Mwenyekiti huyo alitoa agizo kwa baadhi wamiliki wa shule na vyuo visivyo vya Serikali kutotumia kigezo cha pesa ili kudidimiza kiwango cha Elimu nchini.

Kwa upande wake Makamu Mwenyekiti wa shirikisho hilo Bwa. Emmanueli Gwegenyeza ameshauri viongozi na wananchi kwa ujumla kutochanganya suala la Siasa na Elimu kwani kwa kufanya hivyo tutazidi kudidimiza Sekta ya Elimu nchini.


“Tusiingize suala na Siasa na Elimu kwa wakati mmoja kwani kwa kufanya hivyo tunaweza kuididimiza Sekta ya Elimu pia tunaahidi kumpa Waziri ushirikiano ili kuzidi kuinua Sekta ya Elimu nchini,” aliongeza Makamu huyo.

No comments: