Marekani yakiri kuua raia Syria - LEKULE

Breaking

22 May 2015

Marekani yakiri kuua raia Syria


Marekani imekiri, kwa mara ya kwanza kuhusika na mashambulizi ya anga dhidi ya kikosi cha wapiganaji wa kiislamu wa Islamic State yaliyopelekea baadhi ya raia kuuawa.

Katika mkutano wa dharura katika makao makuu ya jeshi la Marekani Pentagon,Luteni Jenerali James Terry ,aliomba radhi kwa vifo vya watoto wawili vilivyotokea bila kukusudiwa mwaka uliopita .

Wakati huohuo rais wa Marekani Barrack Obama amekiri kuwa kutekwa kwa miji ya Palmyra nchini Syria na Ramadi nchini Iraq katika kipindi cha wiki moja iliyopita ni pigo kwa mipango yao lakini sio kushindwa.

Obama ameiambia jarida moja kuwa haamini kuwa serikali yake kwa ushirikiano na serikali iliyoko Iraq zinaelekea kushindwa na makundi ya wapiganaji wa Kisslamu wa Islamic State.

Rais huyo ameahidi kuimarisha maradufu msaada wa kijeshi kwa serikali ya Iraq mbali na kuimarisha mafunzo ya kijeshi kwa wapiganaji wa kisunni .

Wakati huohuo ,Serikali ya Urusi imeahidi kutoa msaada wa hali na mali kwa jeshi la Iraq.

Waziri wa maswala ya kigeni wa Urusi Sergey Lavrov amemuahidi waziri mkuu wa Iraq Haider al-Abadi kuwa Urusi itatekeleza matakwa yote ya Iraq katika jitihada za kuisaidia kukabiliana na wapiganaji wa kisslamu wa Islamic State .

Siku moja baada ya mji wa Syria wa Palmyra kutwaliwa na IS, wakazi wa eneo hilo wanasema waislamu wenye siasa kali bado wanawasaka wale wanaounga mkono serikali.

Wapiganaji wa IS wameripotiwa kuwa wengi zaidi ya maafisa wa ulinzi wa eneo la mashariki mwa Iraq.

IS imetangaza kuundwa kwa himaya yao katika sehemu za Mashariki mwa Iraq na sehemu walizoteka Syria.

No comments: