Afisa wa Intelijensia wa TANAPA Aliuawa na Mfanyakazi Wake Wa Ndani Kwa Kukatwa Panga Wakati Akinywa Uji..... - LEKULE

Breaking

25 Dec 2015

Afisa wa Intelijensia wa TANAPA Aliuawa na Mfanyakazi Wake Wa Ndani Kwa Kukatwa Panga Wakati Akinywa Uji.....


Jeshi la Polisi Mkoani hapa limefanikiwa kumkamata mtu mmoja aitwaye Ismail Swalehe Sang’wa (20) ambaye ni mwenyeji wa kijiji cha Sepuka wilayani Ikungi katika Mkoa wa Singida kwa tuhuma za kumuua Afisa wa Intelijensia wa TANAPA aitwaye Emily Kisamo (52).

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake jana  asubuhi , Kamanda wa Polisi Mkoa wa Arusha Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Liberatus Sabas alisema tukio hilo la mauaji ya Afisa huyo wa TANAPA lilitokea tarehe 18.12.2015 muda kati ya saa 2:30 asubuhi hadi saa 4:00 asubuhi mtaa uitwao Corridor Area Uzunguni jijini  Arusha.

Kamanda Sabas alisema kwamba, siku ya tukio hilo marehemu alikuwa nyumbani kwake sebuleni akiwa anakunywa uji ndipo mtuhumiwa ambaye ni mfanyakazi wake wa ndani  alimvizia na kumkata shingo na kitu kinachoaminika kuwa ni panga na kisha kuchukua mwili wake na kuuweka kwenye gari la marehemu aina ya Nissan Mazda lenye namba za usajili T. 435 CSY.

“Baada ya kuuweka mwili wa marehemu kwenye buti alilisafisha gari hilo kwa nje na kisha kuliendesha mpaka eneo la kikwakwaru “B” kata ya Lemara ambapo alilitelekeza hapo na kisha yeye kuondoka”. Alifafanua Kamanda Sabas.

“Mara baada ya gari hilo kukaa mpaka saa 2:00 usiku ndipo baadhi ya wananchi wa eneo hilo walitoa taarifa kwetu ambapo askari wa doria walikwenda na kulichukua gari hilo kwa kulivuta mpaka kituoni. Kwa kuwa mke wa marehemu aitwaye Caroline Lukumay (38) alikuwa anamtafuta mume wake kwa njia ya simu bila mafanikio ndipo alipoamua kuja kituoni kutoa taarifa ambapo tulimuonyesha gari lililotelekezwa ambalo alillitambua mara moja”. Alisema Kamanda Sabas.

Aliongeza kwa kusema kwamba askari walimuomba mke wa marehemu funguo za akiba za gari hilo ambapo baada ya kulifungua ndipo walipouona mwili wa marehemu kwenye buti akiwa na vitu mbalimbali kama vile simu mbili aina ya Sony na Panasonic, pesa taslimu Tsh 300,000, Laptop aina ya Asus na kadi za benki tofauti tofauti.

Mara baada ya mtuhumiwa huyo kukamatwa alikiri kuhusika na mauaji hayo na kusema siku hiyo walikuwa wawili tu yaani yeye na mrehemu na alifanya hivyo kwa kuwa alikuwa na tamaa za fedha alizokuwa nazo marehemu ndani ya nyumba hiyo kiasi cha Tsh. Mil.5.
 
Upekuzi zaidi wa Jeshi la Polisi ulibaini kuwepo kwa fedha taslimu Tsh. 4,294,000, simu tatu aina ya Sumsang na vocha za mtandao wa vodacom za sh. Elfu tano tano zenye thamani ya Tsh. 70,000 ambapo vyote vilifukiwa kwenye banda la kuku.

Mbali na vitu hivyo pia mtuhumiwa Ismail Swalehe Sang’wa aliweza kuonyesha panga lenye damu ambalo alilihifadhi stoo pamoja na taulo nne kubwa, kitambaa cha mezani na suruali yake ambazo zilikuwa na damu na alizitumia yeye mwenyewe kupigia deki sebuleni baada ya tukio na kisha kuzificha kwenye migomba karibu na mabanda ya kuku.


Kamanda Sabas alimalizia kwa kusema kwamba Jeshi hilo linawashikilia watuhumiwa watatu wengine mbali na Ismail Swalehe Sang’wa akiwemo mke wa marehemu, rafiki wa mke wa marehemu ambaye ni mwanamke na dereva wa nyumbani wa marehemu kwa mahojiano zaidi. 

No comments: