Rais Magufuli Alitaka Baraza Kuu la Waislamu Tanzania- BAKWATA Liombee Taifa Amani - LEKULE

Breaking

27 Jun 2016

Rais Magufuli Alitaka Baraza Kuu la Waislamu Tanzania- BAKWATA Liombee Taifa Amani


Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dakta JOHN MAGUFULI amewahimiza viongozi wa Baraza Kuu la Waislamu Tanzania- BAKWATA- waendelee kuombea amani katika taifa na kukemea ipasavyo vitendo vya uhalifu katika jamii ya Kitanzania.
 
Kauli hiyo ya Rais imetolewa na Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania SAMIA SULUHU HASSAN kwa niaba ya Rais katika tafrija ya futari iliyoandaliwa na Baraza Kuu la Waislamu Tanzania- BAKWATA- katika uwanja wa shule ya sekondari ya KINONDONI MUSLIM jijini Dar es Salaam.
 
Rais Magufuli amesema jamii yeyote inayolelewa na kukua katika misingi ya kufuata maandiko ya Mwenyezi Mungu ni vigumu kujiingiza kirahisi katika vitendo vinavyomchukiza Mungu vikiwemo vitendo vya uhalifu.

Rais MAGUFULI pia amewatakia kheri waumini wote wa dini ya kiislamu kote nchini katika mfungo wa mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
 
Kwa upande wake, Mufti Mkuu wa Tanzania Sheikh ABUBAKAR ZUBEIR ameipongeza serikali kwa hatua inazochukua katika kukabiliana na vitendo vya uhalifu hapa nchini na kusisisita kuwa Viongozi wa BAKWATA na wataendelea kushirikiana na serikali katika kukemea vitendo viovu katika jamii kama hatua ya kuhakikisha vitendo vya uhalifu vinakoma hapa nchini.

Mufti wa Tanzania pia ametoa rai kwa waislamu wote nchini wadumishe umoja,upendo na mshikamano miongoni mwao katika Mfungo wa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani na hata baada ya mfungo kama kitabu kitukufu cha QUR’AN kinavyoelekeza.

Imetolewa na

Ofisi ya Makamu wa Rais.  

No comments: