Jeshi la Polisi Tarime/Rorya Laanza Msako wa Wanaume Wanne Waliombaka Binti Mmoja kwa Zamu na Kumharibu Vibaya - LEKULE

Breaking

1 Apr 2016

Jeshi la Polisi Tarime/Rorya Laanza Msako wa Wanaume Wanne Waliombaka Binti Mmoja kwa Zamu na Kumharibu Vibaya


JESHI la Polisi katika Kanda Maalumu ya Tarime/Rorya mkoani Mara, linawasaka watuhumiwa watano wanaotajwa kuhusika kubaka wasichana wawili katika eneo hilo.

Kamanda wa Polisi wa kanda hiyo, Andrew Satta alisema, watu hao wanatuhumiwa kuwabaka wasichana hao katika matukio mawili tofauti yaliyotendwa kwa nyakati tofauti Machi 26, mwaka huu katika wilaya za Rorya na Tarime.

Satta alisema kuwa, katika tukio la kwanza mwanafunzi wa shule ya msingi Kibasisi iliyopo kwenye kijiji cha Kangariani wilayani Tarime (Jina limehifadhiwa), alibakwa na watu wawili wakati akirejea nyumbani kutoka shuleni siku hiyo ya Machi 26.

Kamanda Satta alisema kuwa, mwanafunzi huyo alikutana njiani na watu wawili waliokuwa wamejifunga vitambaa vyeusi usoni, ambao walimkamata kwa nguvu, kumburuza vichakani na kumbaka kwa zamu. Alieleza zaidi kuwa, baada ya kumbaka, watu hao walimdhibiti asipige kelele kwa kumfunga kitambaa mdomoni.

“Walipomaliza kumbaka walitokomea kwenye vichaka na kutorokea mahali pasipojulikana, lakini Polisi inawasaka,” alisema na kuongeza kuwa, tukio hilo liliripotiwa Polisi na mwanafunzi huyo.

Katika tukio la pili, Kamanda Satta alisema kuwa, siku hiyo usiku kwenye kijiji cha Ruhu kwenye mwalo wa wavuvi wilayani Rorya, msichana mwenye umri wa miaka 21 (Jina limehifadhiwa), alidanganywa na vijana wanne kuwa aliitwa na rafiki yake wa kiume, jambo lililomfanya awaombe wamsindikize alipo na walitii.

Kamanda Satta alisema kuwa, bila kujua nia ya vijana hao kumdanganya hivyo, binti huyo ambaye hata hivyo anawatambua na kufahamu majina yao, alikubali na kuondoka nao. 
Alisema kuwa baada ya kufika kwenye eneo la mwalo wa wavuvi, karibu na vichaka, huku kukiwa na giza nene, waliamua kumkamata kwa nguvu na kumfunga mdomo kwa kitambaa asiweze kupiga kelele.

“Walipofanikiwa kudhibiti asipige kelele vijana hao wanne walimbaka kwa zamu na kumwacha akiwa hoi vichakani, ndipo binti huyo alipoamua kujikongoja hadi kwenye eneo alipopata msaada wa wasamaria waliomsindikiza kutoa taarifa kwenye kituo cha Polisi na kwenda hospitali kwa matibabu”, alisema.

Watu hao waliotajwa na binti huyo kuwa ndio waliombaka ni pamoja na Ophia Robert ambaye amekamatwa, Nchama Bureki, Robert Shija na mwingine aliyetajwa kwa jina moja, Mashije. 

Aliwaonya wanaoendeleza ubakaji katika kanda hiyo kuacha kwa sababu msako unaofanywa ni endelevu na jeshi hilo halitasita kuwachukulia hatua za kisheria.

No comments: