Zitto Kabwe Amuomba Rais Magufuli Atengue Agizo la Jakaya Kikwete - LEKULE

Breaking

6 Mar 2016

Zitto Kabwe Amuomba Rais Magufuli Atengue Agizo la Jakaya Kikwete


Mbunge wa Jimbo la Kigoma Mjini, Zitto Kabwe anatafuta nafasi ya kukutana na Rais John Magufuli kumuomba atengue agizo la Rais Jakaya Kikwete la kuzuia ujenzi wa makazi katika Mlima wa Mlole Manispaa ya Kigoma Ujiji.

Rais Kikwete alitoa agizo hilo mwaka 2006 kama moja ya hatua za kudhibiti mmomonyoko wa ardhi na kujaa mchanga kwa bandari ya Kigoma.

Akizungumza kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja vya Kigoma Cinema mjini Kigoma, Mbunge huyo alisema ameamua kuchukua hatua hiyo kwa kuamini kwamba taarifa alizopewa Rais Kikwete zilizosababisha kutoa agizo hilo hazikuwa sahihi.

Zitto alisema Rais Kikwete alipewa taarifa potofu kwamba mmomonyoko wa udongo kutoka katika eneo hilo ndiyo unaosababisha kujaza mchanga na kupunguza kina katika bandari ya Kigoma.

Mbunge huyo wa Kigoma Mjini alisema kuwa tafiti zilizofanyika na taarifa zilizopo zinaonesha kuwa kupanuliwa kwa Mto Lukuga kunafanya maji kutoka kwa wingi na kuingia bahari ya Atlantiki ndiko kulikochangia kupunguza kina cha maji katika maeneo mbalimbali ya mwambao wa Ziwa Tanganyika.

Kwa mujibu wa tathmini iliyofanywa mwaka 2008 inaonyesha kuwa kiasi cha Sh bilioni tano kilikuwa kikihitajika kwa ajili ya kuwalipa fidia wakazi hao, fedha ambazo uongozi wa Halmashauri ya Manispaa ya Kigoma Ujiji imesema haiwezi kuzilipa hivyo kutaka mamlaka za serikali kuona namna ya kutafuta fedha hizo na kugharamia kuwalipa watu hao.


Wakizungumzia kauli ya Zitto, baadhi ya wakazi wa eneo la Mlole ambao wameathirika kwa kiasi kikubwa na agizo hilo la Rais Kikwete, walisema kuwa wameanza kupata matumaini ya kuona thamani ya nyumba zao kwani tangu kutolewa kwa agizo hilo nyumba zao zimekuwa hazina thamani mahali popote.

No comments: