Tanesco Yaomba Kupandisha Bei ya Umeme. - LEKULE

Breaking

27 Feb 2016

Tanesco Yaomba Kupandisha Bei ya Umeme.



SHIRIKA la Umeme (Tanesco) limepeleka maombi kwa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura), kuomba kupandisha bei ya nishati hiyo, kinyume na matakwa ya Waziri wa Nishati na Madini, Profesa Sospeter Muhongo ya kushusha bei hiyo.
 
Taarifa ya Ewura kwa umma iliyotolewa kwenye vyombo vya habari jana, imeeleza kuwa maombi hayo yamepokewa Jumatano ya wiki hii na kutaka wadau kujitokeza kujadili uhalali wa nyongeza hiyo siku mkutano huo utakapoitishwa.
 
“Mamlaka inaanzisha mchakato wa kupata maoni ya wadau, ili kujua uhalali wa maombi ya nyongeza ya bei za huduma iliyoyapokea kutoka Tanesco,” imeeleza taarifa hiyo.
 
Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Tanesco iliwasilisha ombi husika kulingana na Sheria ya Umeme namba 131, inayoitaka Ewura kufanya mabadiliko ya bei zinazotozwa na mtoa huduma mara moja kila baada ya miaka mitatu.
 
“Pendekezo la wastani wa badiliko la bei za umeme ni asilimia 1.1 kuanzia Aprili mosi 2016 na asilimia 7.9 kuanzia Januari mosi 2017,”limeeleza tangazo hilo.
 
Mapendekezo hayo japo ya kisheria, lakini yanapingana na msimamo wa Waziri Muhongo, ambaye tangu alipoapishwa kushika wadhifa huo, alielezea kusudio lake la kutaka bei ya nishati hiyo ishushwe.
 
Profesa Muhongo alikwenda mbali na kuagiza Tanesco, Ewura na Shirika la Maendeleo ya Petroli (TPDC), kumpelekea mapendekezo ya kushuka kwa bei ya umeme kuanzia mwanzoni mwa mwaka huu.
 
Katika maagizo hayo, Profesa Muhongo alihoji kwa nini bei ya umeme isishuke, wakati gharama za uzalishaji wa umeme wa kutumia mafuta zimeshuka kutokana na kupungua kwa bei ya mafuta katika soko la dunia.
 
Kutokana na maombi hayo ya Tanesco, Ewura imewataka wadau wa nishati wanaopenda kutoa maoni yao kwa maandishi, kufanya hivyo kwa kutuma maoni yao kwa Mkurugenzi Mkuu wa Ewura, ghorofa ya saba jengo la LAPF Pensions Fund Tower, mkabala na Kijiji cha Makumbusho, Kijitonyama Dar es Salaam.
 
Kwa watakaotuma kwa njia ya posta, wameombwa kufanya hivyo kwa kutumia Sanduku la Posta 72175, Dar es Salaam, Tanzania, simu namba (+255-22) 2123853-4; Fax namba (+255-22) 2123180; Barua pepe info@energyregulators.org au tovuti http://www. energyregulators. org.
 
Taarifa hiyo imeeleza kuwa mamlaka hiyo pia, itaitisha mikutano ya wazi ili kukusanya maoni kuhusu mapendekezo hayo kutoka kwa wadau mbalimbali, wakiwamo Baraza la Wawakilishi wa Watumiaji wa Huduma (CCC); Baraza la Ushauri la Serikali (GCC) pamoja na wananchi kwa ujumla.

No comments: