Sherehe za Miaka 39 ya CCM: Rais Magufuli Atuma Salamu Kwa Watendaji Wavivu Serikalini - LEKULE

Breaking

7 Feb 2016

Sherehe za Miaka 39 ya CCM: Rais Magufuli Atuma Salamu Kwa Watendaji Wavivu Serikalini



Rais John Magufuli amewataka watendaji wote wa serikali kuhakikisha kuwa wanatekeleza ipasavyo matakwa ya ilani ya Chama Cha Mapinduzi kwa kuwa ndicho kinachoongoza nchi kwa sasa.

Magufuli ametoa agizo hilo leo kwenye sherehe za miaka 39 ya kuzaliwa kwa Chama cha Mapinduzi zilizofanyika katika uwanja wa Namfua mjini Singida.

Rais Magufuli ambaye alikuwa ni miongoni viongozi wakuu wa serikali waliohudhuria sherehe hizo akiambatana na makamu wake Samiah Suluhu Hassan na Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, amesema yeye na serikali yake wamejipanga kutekeleza kikamilifu ilani ya CCM na kwamba hawezi kukiangusha chama hicho.

Akitoa salam zake katika sherehe hizo, Magufuli ametumia muda usiozidi dakika 10 kueleza mambo ambayo tayari serikali yake imeanza kuyafanya na ambayo itaendelea kuyafanya ikiwa ni pamoja na "kutumbua majipu" kwa ustawi wa maisha ya watanzania wote bila kujali vyama vyao.

Ametumia nafasi hiyo kuwaagiza wakuu wa mikoa, wakuu wa wilaya pamoja na watendaji wote serikalini kufanya kazi kwa nguvu, uadilifu na uzalendo ili kuwaletea watanzania maendeleo, na kwamba atakayeona hawezi atamuweka pembeni ili wengine wafanye kazi.

“Nawaeleza watendaji wote serikalini kuwa atakayeshindwa kufanya kazi, nitamueleza kwa upole sana maana mimi ni mtu mpole, nitamuambia akae pembeni apishe wengine”

Rais Magufuli pia ameupongeza uongozi wa CCM mkoa wa Singida kwa kuchangia madawati 1000 kwa shule za Singida na kuwaagiza wakuu wote wa mikoa na wilaya kuhakikisha wanafunzi hawakai chini.

“Mh mwenyekiti inasikitisha sana kuona sisi tunajifungia kwenye maofisi makubwa yenye viyoyozi, na maviti ya kuzunguka lakini tukitoka tu nje tunakuta wanafunzi wamekaa chini kwenye mavumbi, sasa nawaagiza wakuu wa wilaya na wakuu wa mikoa hakikisheni wanafunzi hawakai chini”

Rais Magufuli pia ametumia nafasi hiyo kukishukuru Chama cha Mapinduzi kufanikisha yeye kuwa Rais kwa kuwa bila chama hicho yeye asingekuwa Rais.

“Nataka watanzania wote wajue kuwa bila CCM mimi nisingekuwa Rais wao, kwa hiyo huwezi kunitenganisha mimi na CCM, ndiyo maana leo nimekuja nimevaa kijani yangu hapa”

Pia amesema haoni kama kuna chama kingine chochote kitakachokuja kutawala Tanzania zaidi ya CCM

"Nataka ifikie hatua watanzanie wote wasiwaze wala kuota vyama vingine, tutafanya yale ambayo wao wanataka kuyafanya, ... Hakuna mtawala anayetaka kutawaliwa, tena kwa bahati mbaya atawaliwe na vyama vya hovyohovyo, CCM itaendelea kutawala"

No comments: