Mke Wa Kafulila ( Jesca Kishoa ) Ataka Dr. Mwakyembe Naye Akamatwe Na Kufikishwa Mahakamani Kwa Kuhusika Na Sakata La Mabehewa Mabovu - LEKULE

Breaking

15 Feb 2016

Mke Wa Kafulila ( Jesca Kishoa ) Ataka Dr. Mwakyembe Naye Akamatwe Na Kufikishwa Mahakamani Kwa Kuhusika Na Sakata La Mabehewa Mabovu



Mbunge wa Viti Maalumu, mkoani Singida Jesca Kishoa(CHADEMA), amesema aliyekuwa Waziri wa Uchukuzi, Dkt. Harrison Mwakyembe na Katibu Mkuu wake, wanapaswa kufikishwa mahakamani katika sakata la mabehewa mabovu.

Akizungumza jana jijini Dar es Salaam,  Kishoa alisema viongozi hao, pia aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha wakati huo, naye afikishwe mahakamani kwa sababu ndiye alikuwa mlipaji Mkuu wa Serikali.

Alisema ni aibu Kiti cha Spika kumfukuza mbunge bungeni akidaiwa kuzungumza uongo kabla ya kudai ripoti ya mabehewa ili kujua ukweli wa jambo hilo ni upi.

Aliongeza kuwa, Katibu Mkuu huyo alilipa fedha asilimia 100 kinyume cha sheria wakati Dkt. Mwakyembe ambaye kwa sasa ni Waziri wa Katiba na Sheria, aliruhusu mabehewa yanunuliwe.

"Aliyekuwa Katibu Mkuu Wizara ya Uchukuzi naye awajibishwe kwa kosa hilo kama Mtendaji Mkuu wa Wizara...mabehewa hayo yalipokewa kwa mbwembwe lakini kasoro zake zinatokana na zabuni ya utengenezaji wake kutozingatia viwango.

"Kampuni ya Hindustan Engineering haikufanyiwa uchunguzi kuhusu rekodi na uwezo wake, malipo yalifanyika kwa asilimia
100 kabla ya mabehewa hayajawasili nchini," alisema.

Alisema umma unashuhudia baadhi ya vigogo wa TRL wanafikishwa mahakamani kutokana na sakata la mabehewa hayo na kusisitiza sheria ichukue mkondo wake kwa wote waliohusika si  kuwashtaki wachache wakati Mawaziri wanaachwa.

Kishoa ambaye ni Mke wa aliyekuwa Mbunge wa Kigoma Kusini David Kafulila (NCCR-Mageuzi), alisema hakuna mtu mwenye uhakika kwamba mabehewa mabovu ni 25 kati ya 275.

"Nani ana uhakika kwamba waliokamatwa ndio wanahusika peke yao, haiwezekani Serikali ikajichunguza yenyewe, kujishughulikia yenyewe kwa kuamua nani imtoe kafara, nani imlinde wote, wote washtakiwe kama ilivyo kwa wengine," alisema Kishoa.

Kishoa alihoji kwanini ripoti ya mabehewa inaendelea kufichwa na haifikishwi bungeni ili Bunge liweze kuisimamia Serikali jambo ambalo halitoi picha kwa Bunge la 11.

No comments: