Diwani Wa CUF Auawa Kwa Kucharangwa Mapanga Na Watu Wasiojulikana - LEKULE

Breaking

2 Feb 2016

Diwani Wa CUF Auawa Kwa Kucharangwa Mapanga Na Watu Wasiojulikana


Diwani wa kata ya Kimwani iliyoko Wilaya ya Muleba Mkoani Kagera, Silvester Miga (CUF) amepoteza maisha baada ya kuvamiwa na kukatwa na mapanga nyumbani kwake, usiku wa kuamkia jana.

Kamanda wa Polisi Mkoani Kagera, Augustine Ollomi alithibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa marehemu alipoteza maisha majira ya saa saba usiku akiwa anapatiwa matibabu katika hospitali ya Kagondo.

Imeelezwa kuwa Miga alivamiwa nyumbani kwake akiwa anaangalia taarifa ya habari kwenye runinga ambapo watu hao walimvamia na kutekeleza tukio hilo la kikatili.

Kamanda Ollomi alisema kuwa Jeshi la Polisi mkoani humo limeendesha msako mkali na kuwakamata watu wawili wanaotuhumiwa kuhusika na tukio hilo.

 Aliwataja watu hao kuwa ni Aderarid Antony mwenye umri wa miaka 42 na Shiranga Gonzari mwenye umri wa miaka 22.

Baadhi ya wakazi wa kata Kimwani waliwaambia waandishi wa habari kuwa mazingira ya kuuawa kwa diwani wao ni ya kisiasa zaidi.

No comments: