Waziri Muhongo aahidi kuongeza matumizi ya umeme wa makaa ya mawe - LEKULE

Breaking

13 Jan 2016

Waziri Muhongo aahidi kuongeza matumizi ya umeme wa makaa ya mawe



Serikali imesema itahakikisha makaa ya mawe yanakua chanzo kingine kikubwa cha uzalishaji wa umeme nchini ili kupunguza gharama za umeme zilizopo hivi sasa.

Waziri wa Nishati na Madini, Prof. Sospeter Muhongo ameyasema hayo  alipotembelea mgodi wa makaa ya mawe wa Ngaka uliopo wilaya ya Mbinga mkoani Ruvuma na kuongeza kuwa serikali itahakikisha inafanya kazi kwa ushirikiano mkubwa na mgodi huo ili kuimarisha uchumi wa taifa kupitia makaa ya mawe.

“Nimeelezwa makaa ya Ngaka yana  ubora na kiwango cha hali ya juu na nimeelezwa  kwamba kuna baadhi ya viwanda vimeingia mkataba na Ngaka lakini  badala yake wananunua makaa kutoka nje. Hilo halikubaliki ikiwa makaa ya ndani ya nchi yana ubora lazima tutumie bidhaa za nyumbani,”amesisitiza Prof. Muhongo.

Kutokana na malalamiko ya Mgodi kuhusu hali ya Mkataba ya kuuziana makaa kutoafikiana, Waziri Muhongo ameutaka mgodi huo,Shirika la Maendeleo ya Taifa (NDC),EWURA, Kampuni za Saruji za Dangote, Tanga Cement na Shirika la Umeme Nchini (TANESCO) kukutana Makao Makuu ya Wizara tarehe 14 Januari,2016, ili kujadili  kuhusu suala hilo na pia kujadiliana juu ya  gharama za kuuziana umeme na TANESCO pindi mgodi huo utakapoanza kuzalisha umeme kwa kutumia makaa ya mawe.

Kwa mujibu wa Mkuu wa Masoko wa mgodi wa Ngaka, Christopher Temba, mgodi huo unazalisha tani za makaa ya mawe laki tano kwa mwaka na tayari makaa hayo yanasafirishwa katika nchi za Kenya, Zambia, Malawi na vilevile katika viwanda kadhaa hapa nchini vikiwemo vya  Saruji, Mohamed Enterprises na viwanda vingine.

No comments: