Waziri Mkuu Mstaafu ,Mizengo Pinda Awafunda Wabunge Wa CCM.....Awataka Kujenga Hoja Vizuri Ili Kuwakabili Wabunge Wa Upinzani - LEKULE

Breaking

21 Jan 2016

Waziri Mkuu Mstaafu ,Mizengo Pinda Awafunda Wabunge Wa CCM.....Awataka Kujenga Hoja Vizuri Ili Kuwakabili Wabunge Wa Upinzani


WAZIRI Mkuu mstaafu, Mizengo Pinda amewataka wabunge wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kujenga hoja vizuri katika Bunge linalotarajia kuanza vikao vyake wiki ijayo mjini Dodoma, kwa kuwa wabunge wa vyama vya upinzani wameongezeka bungeni.

Hayo yalisemwa jana Dar es Salaam na Pinda, baada ya kuaga mwili wa aliyekuwa Mbunge wa Viti Maalumu, Leticia Nyerere, aliyefariki akiwa Maryland nchini Marekani akipatiwa matibabu.

Akizungumzia Bunge la sasa, Pinda aliwashauri wabunge wanaounda Bunge hilo ambao wengi wao ni vijana, kuzingatia maslahi ya taifa na sio itikadi za vyama vyao na kuwasisitiza wabunge wa CCM, kujipanga na kwenda na hoja.

“Kila upande ujiandae kwenye kuwasilisha hoja, kuna ongezeko la wabunge wa upinzani, sasa wabunge wa CCM ni lazima nao wajipange na kujenga hoja vizuri,” alisema Pinda. 

Alisema kwa mtazamo wake, Bunge ni zuri na sio la mivutano kwa kuwa kila mmoja amejipanga kuwasilisha hoja zitakazomgusa mwananchi kwa lengo la kumsaidia.

Akizungumzia utawala wa Awamu ya Tano wa Rais John Magufuli, Pinda alisema kila zama zina kitabu chake; na kwa utawala wa Rais Magufuli ameanza vizuri na kuomba Watanzania kumuunga mkono ili kufanikisha azma ya maendeleo ya taifa.

Alisema katika uongozi wake, ndio muda wa kuhakikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo inayoisha baada ya miaka 10 ijayo, inapaswa kuwa imetekelezwa, hivyo hatua mbalimbali anazozifanya rais, ikiwa ni pamoja na kubana matumizi, ni mambo muhimu.

“Hatua zinazofanywa na Rais Magufuli ni za msingi katika kuhakikisha dira ya Taifa ya Maendeleo inatekelezwa, ni vyema Watanzania wote tumuunge mkono juhudi zake”, alisema Waziri Mkuu mstaafu Pinda.


No comments: