Wapambe Wa Wassira Kukata Rufaa Kupinga Hukumu Ya Mahakama Kuu Iliyohalalisha Ushindi Wa Esther Bulaya - LEKULE

Breaking

27 Jan 2016

Wapambe Wa Wassira Kukata Rufaa Kupinga Hukumu Ya Mahakama Kuu Iliyohalalisha Ushindi Wa Esther Bulaya


Baada ya Mahakama Kuu ya Tanzania, Kanda ya Mwanza, kuipiga chini kesi iliyokuwa ikimkabili mbunge wa Bunda Mjini (Chadema), Esther Bulaya, wadai katika kesi hiyo wanatarajiwa kupinga uamuzi huo  Mahakama ya Rufani.

Mwanasheria wa wadai hao, Constantine Mutalemwa, jana alisema wateja wake hawajaridhika na hukumu hiyo iliyotolewa na Jaji Gwae.

Juzi katika mahakama hiyo, Bulaya aliwashinda wakazi wanne wa jimbo hilo waliofungua kesi ya kumpinga baada ya ushindi alioupata kwenye uchaguzi mkuu wa Oktoba 25, mwaka jana. Katika uchaguzi huo, Bulaya olimshinda mpinzani wake, Stephen Wasira wa CCM.

Bulaya, katika kesi hiyo, alikuwa akitetewa na mwanasheria maarufu, Tundu Lissu.

Waliofungua kesi hiyo ni Magambo Masato, Matwiga Matwiga, Janes Ezekiel na Ascetic Malagira, ambao walikuwa na mawakili wawili ambao ni Mutalemwa na Denis Kahangwa.

Mutalemwa alisema baada ya kutoridhika na uamuzi huo, wateja wake wamekusudia kufungua kesi Mahakama ya Rufani ili kupata ufafanuzi wa Jaji juu ya uhalali wao wa kutokuwa na mamlaka kisheria ya kufungua kesi kama hiyo.

Katika hatua nyingine, kesi ya madai iliyofunguliwa katika Mahakama Kuu Kanda ya Mwanza na mbunge wa zamani wa Nyamagana (Chadema), Hezekiah Wenje, jana iliahirishwa hadi Februari 2, mwaka huu.


Uamuzi wa kuahirisha kesi hiyo, ulitolewa na Jaji Joaquine De Mello wa mahakama hiyo, aliposikiliza kwa muda kabla ya kupangiwa jaji wa kuisikiliza kesi hiyo ya kupinga ushindi wa Stanslaus Mabula (CCM).

No comments: