WAFANYAKAZI 350 WA KIWANDA CHA SUKARI CHA MAHONDA WAKOHATARINI KUPOTEZA AJIRA ZAO. - LEKULE

Breaking

4 Jan 2016

WAFANYAKAZI 350 WA KIWANDA CHA SUKARI CHA MAHONDA WAKOHATARINI KUPOTEZA AJIRA ZAO.

 Baadhi ya Miwa iliyoteketea kwa moto kutokana na hujuma iliyofanywa na Watu wasiojuilikana huko kwenye mashamba ya Miwa ya Kiwanda cha Sukari Mahonda Mkoa wa Kaskazini Unguja.
 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akimpa Pole Meneja wa Mradi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda Bwana Tushar Mehta kufuatia watu wasiojuilikana kutia tena moto mashamba ya Miwa Mahonda.
  Balozi Seif kati kati akifuatana na Uongozi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda akikagua baadhi ya sehemu ya shamba la Miwa la Eka 50 lililotiwa moto jana jioni na watu wasiojuilikana.
Wa kwanza kulia ni Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Meja Mstaafu Juma Kassim Tindwa.
 Meneja wa Mradi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda Bwana Tushar Mehta akimueleza Balozi Seif hasara iliyopatikana kutokana na hujuma ya moto kwenye mashamba ya Miwa Mahonda.
Balozi Seif akielezea masikitiko yake kutokana na baadhi ya watu kufanya hujuma za makusudi kujaribu kuvuruga juhudi za Uongozi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda za kuimarisha Sekta ya Viwanda.


TISHIO la ajira za Wafanyakazi 350 wa Kiwanda cha Sukari Mahonda zinaendelea kuwa hatarini kufuatia hujuma zinazofanywa kwa makusudi na baadhi ya watu kuendelea kutia moto mashamba ya miwa huko Mahonda Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Kitendo hicho cha hujuma kinaweza kuusababisha Uongozi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda kuwa na mawazo ya kufikiria kuzuia ajira mpya 450 za Wafanyakazi wa Kiwanda hicho katika malengo yake baada ya kukamilika kwa matengenezo makubwa na kuanza tena uzalishaji wa sukari.
Meneja wa Mradi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda Bwana Tushar Mehta alisema hayo wakati akimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi aliyefika kuangalia hasara iliyosababishwa na moto uliotiwa kwa mara nyengine tena na Watu wasiojuilikana ndani ya shamba la Miwa katika kipindi cha siku Tano baada ya tukio kama hilo la Tarehe 30 mwezi uliopita.
Bwana Tushar alisema moto huo umetiwa kati kati ya shamba la Miwa jana jioni na wahalifu wenye dhamira ya makusudi ya kutoa usumbufu na kizuizi kwa wananchi na vikosi vya Ulinzi katika harakati za kukabiliana na moto huo. .
Alisema Eka zipatazo 50 za Miwa iliyopevuka imeteketea kwa moto hali ambayo imeisababishia Kiwanda hicho hasara ya Tani 200 za Sukari na Lita 2,300 za Spititi zilizokuwa zizalishwe kutokana na miwa hiyo ikiwa na hasara ya jumla ya dola za Kimarekani Laki 228,758.56 sawa na zaidi ya shilingi Milioni 494 za Kitanzania.
Meneja huyo wa Mradi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda alifahamisha kwamba hadi sasa Eka zipatazo 200 zimeteketea kwa moto kwenye matukio yote mawili katika kipindi cha siku Tano zilizopita na kusababisha hasara ya jumla ya Dola za Kimarekani Milioni 1,176,234.28 sawa na shilingi za Kitanzania Bilioni 2,326,818,500/-.
Akiupa pole Uongozi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda kutokana na hasara ya Mashamba iliyosababishwa na moto huo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alisema hujuma hiyo ya makusudi haiitakii neema Zanzibar katika harakati zake za kustawisha uchumi wake.
Balozi Seif aliwanasihi watu wenye tabia hiyo kuachana nayo kwani mbali ya kujibebesha dhambi lakini pia inawavunja moyo wawekezaji walioamua kuja kuwekeza miradi yao ya kiuchumi Nchini kwa lengo la kuisaidia Serikali pamoja na Wananachi hapa Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alifahamisha kwamba juhudi za makusudi za Serikali kuu katika kukifufua tena Kiwanda cha Sukari na Manukato Mahonda baada ya kusita kwa miaka kadhaa zililenga kuimarisha  Uchumi kupitia sekta ya viwanda sambamba na kupanua soko la ajira kwa Vijana.
Alisema tabia ya baadhi ya watu kufikiria kwamba hujuma hiyo itatoa fursa kwao kutumia maeneo ya mashamba ya Miwa kuendeleza Kilimo na Mifugo inafaa kuachwa mara moja kwa vile mashamba hayo yataendelea kuwa katika mipango ya Serikali ya kuhudumia Sekta ya Viwanda.
“ Haya ni Mashamba ya Serikali yaliyotengwa maalum kwa shughuli za harakati za Viwanda. Hivyo ndoto za baadhi ya Watu kufikiria kwamba hujuma zao zitazaa matunda kwa kufanya wanavyotaka zinapaswa ziachwe mara moja ”. Alisema Balozi Seif.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar aliufahaisha Uongozi wa Kiwanda cha Sukari Mahonda kwamba Serikali Kuu inaangalia mpango utakaowezesha Vikosi vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kusaidia ulinzi kwenye Mashamba hayo ili kulinda hujuma zinazoonekana kushamiri siku hadi siku.
Hilo ni tukio la sita la hujuma za moto kwenye mashamba ya Miwa ya Kiwanda cha Sukari Mahonda tokea kianze tena uzalishaji wa sukari na Spiriti mapema mwaka uliopita wa 2015.
Othman Khamis Ame
Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar
4/1/2016.

No comments: