UVCCM Mkoa wa Vyuo Wampa Makavu Benard Membe Kwa Kumponda Rais Magufuli - LEKULE

Breaking

24 Jan 2016

UVCCM Mkoa wa Vyuo Wampa Makavu Benard Membe Kwa Kumponda Rais Magufuli


SHIRIKISHO LA VYUO VYA ELIMU YA JUU
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI

Ndugu waandishi wa habari, nimewaita hapa kuelezea masikitiko makubwa kutokana na kauli za hivi karibuni za aliyekuwa waziri wa mambo ya nje ndugu Bernard Membe.

 Akifanya mahojiano na kunukuliwa na gazeti la Mwananchi la tarehe 22 na 23 Januari, 2016 , ndugu Membe amekaririwa akitoa kauli zenye maudhui ya kubeza juhudi za mh. Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Dr. John Magufuli na kufutwa kwa uchaguzi wa Zanzibar. Kauli hizi zilijikita katika maeneo makubwa manne kama ifuatavyo:-

1. Ndugu Membe amebeza juhudi za Rais Dr. John Magufuli za kupunguza ukubwa wa serikali, na kwamba hatua yake ya kupunguza ukubwa wa baraza la mawaziri haijasaidia chochote kwa taifa. Na kwamba ni sawa na kupunguza idadi ya mifuko huku idadi ya mayai ikiwa ni ile ile.

2. Ndugu Membe amekosoa na kubeza hatua ya serikali ya awamu ya tano chini ya Rais Dr. Magufuli ya kupunguza safari za nje zisizo za lazima na tija kwa taifa, na kwamba safari hizo zilikua na neema kubwa kwa watanzania.

3. Ndugu Membe amepinga kufutwa kwa matokeo yote ya uchaguzi visiwani Zanzibar na kudai kwamba dunia nzima inatushangaa kwa uamuzi huo.

4. Ndugu Membe amekosoa mazungumzo ya kutafuta maridhiano baina ya Chama cha CUF na CCM visiwani Zanzibar huku akidai kuwa ni makosa kuwaachia Rais wa Zanzibar Dr. Ali Mohammed Shein na Maalim Seif Shariff Hamad kufanya mazungumzo peke yao.

Tumesikitishwa sana na kauli hizo na vijana wasomi tumeamua kumjibu kama ifuatavyo:-

KUPUNGUZA UKUBWA WA SERIKALI
Rais Dr. John Magufuli amechukua juhudi za kupunguza ukubwa wa serikali kwa kuanza na baraza la mawaziri.

 Idadi ya mawaziri imepungua kutoka mawaziri 60 wakati wa serikali ya awamu ya nne hadi mawaziri 34 tu katika serikali ya awamu ya tano. Punguzo hili ni idadi ya mawaziri 26.

Gharama za kawaida za kumuhudumia waziri zilizopungua:
a. Kila waziri na naibu wake hupewa gari aina ya GX V8 ambalo thamani yake inakadiriwa milioni 400. Gari hili linahitaji mafuta na gharama ya kulitunza. Hivyo magari 26 yamepungua ambayo gharama yake ya manunuzi na matunzo ni mabilioni ya pesa.

b. Nyumba ya kuishi. Mawaziri wote wanapewa nyumba na serikali. Nyumba hizo zinalipiwa umeme na maji

c. Wasaidizi wa mawaziri. Kila waziri anapewa katibu wake, hivyo serikali imepunguza nafasi 26 za makatibu kwa kupunguza mawaziri 26. Hawa wanalipwa mishahara na posho.

d. Madereva. Kila waziri ana dereva wa serikali anayelipwa mshahara na posho awapo nje ya kituo cha kazi. Hivyo serikali imepunguza mishahara na posho za watu 26.

e. Kila waziri anapewa ulinzi nyumbani kwake wa askari wawili wa jeshi la polisi masaa 24. Hivyo kwa kupunguza mawaziri 26, tumepunguza askari 52 ambao sasa watakwenda kuongeza ulinzi wa raia na mali za wananchi wengine.

f. Kila waziri anatengewa mafungu ya fedha kwa ajili ya mawasiliano, safari zake za kikazi, ziara za mikoani, vikao na majukumu mengine ya kazi ambayo ni mamilioni ya shilingi kila mwezi. Kwa kupunguza mawaziri 26 Rais ameokoa mamilioni ya shilingi kila mwezi.

g. Gharama za kuwahudumia mawaziri 26 wakiwa bungeni Dodoma pia zimepungua.

WIZARA ZILIZOUNGANISHWA
Katika muundo wa baraza la mawaziri la Dr. John Pombe Magufuli alilolitangaza , ziko wizara 5 ambazo zimeunganishwa pamoja. Wizara hizi ni

a. Kilimo, Mifugo na Uvuvi (wizara 3 zimeunganishwa, sasa zina waziri 1)-Mh. Mwigulu Nchemba

b. Wizara ya mambo ya nje, kikanda na kimataifa (wizara mbili zimeunganishwa, sasa zina waziri 1)- Mh. Augustine Mahiga

c. Wizara ya viwanda, biashara na uwekezaji (wizara 2 zimeunganishwa,sasa zina waziri 1)- Mh. Charles Mwijage

d. Wizara ya elimu, sayansi, teknolojia na ufundi (wizara 2 zimeunganishwa, sasa zina waziri 1)- Mh. Joyce Ndalichako

e. Wizara ya ujenzi, mawasiliano na chukuzi (wizara 3 zimeunganishwa, sasa zina waziri 1) -Mh. Makame Mbarawa

Katika hali hiyo, ni dhahiri idadi ya mawaziri imepungua na hivyo gharama ya kuwahudumia pia imepungua. Kutoka hadharani na kusema hakuna kilichopungua ni upotoshaji mkubwa ambao mtu mwenye uelewa wa kawaida kabisa anaweza kuubaini.

IDADI YA MAKATIBU WAKUU
Makatibu wakuu na manaibu waliohudumu wizara wakati wa serikali ya awamu ya nne walikuwa jumla ni 54. Mh. Rais Dr. Magufuli ameteua makatibu wakuu 29 na manaibu 21. Hivyo hapa pia idadi imepungua na kufanya gharama kupungua pia.

WATANZANIA WANAMSHANGAA MEMBE
Kitendo cha ndugu Bernard Membe kudai kuwa kupungua huku kwa ukubwa wa baraza la mawaziri hakujasaidia kupunguza gharama za uendeshaji wa serikali, ni jambo la ajabu ambalo watanzania wote wanalishangaa na kuliona kuwa ni uongo na upotoshaji mkubwa. Upotoshaji huu unastahili kupuuzwa na kila mpenda mabadiliko ya kweli.

Baada ya Mh. Raisi kuteua baraza lake la mawaziri mwezi desemba, mwanazuoni profesa Samuel Wangwe alikaririwa na gazetila Habari Leo la tarehe 11 Desemba, 2016 akisifu Mh. Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dr. John Magufuli kupunguza idadi ya mawaziri. 

Profesa Wangwe alisema mawaziri ni watu wa kusimamia sera, na watendaji wakubwa ni makatibu wakuu. Aidha, wanaharakati na wadau mbalimbali wote walipongeza kupunguzwa huko kwa baraza la mawaziri wakisema taifa limepunguza mzigo. Lakini ajabu, ndugu Bernard Membe hajaliona hilo. Inasikitisha sana.

Wakati mwingine inatufanya tujiulize, ndugu Membe ambaye alikua miongoni mwa wana CCM waliowania kuteuliwa na Chama kugombea Urais wa Tanzania, na baadae kushindwa kwa kura ndani ya Halmashauri Kuu ya CCM taifa, amesema maneno haya kwa malengo au makusudio yapi?

Waswahili wanasema, aliyepata kapata. Tunamtaka ndugu Membe ajiunge na watanzania kukubali kuwa Dr. Magufuli ndiye Rais wa nchi yetu aliyechaguliwa na wananchi. Hivyo amuache atimize wajibu wake kwa taifa.

KUPUNGUZA SAFARI ZA NJE
Katika hatua nyingine ya kupunguza matumizi yasiyo ya lazima serikalini, Raisi ameagiza kufutwa kwa safari zote zisizo za tija kwa nchi, na kwamba safari zote zitatolewa kwa kibali maalum cha Raisi.

Kwa mujibu wa hotuba ya Rais wa jamhuri ya muungano wa Tanzania Dr. John Magufuli bungeni mjini Dodoma, safari za nje za miaka miwili pekee (2013-2015) ndugu Membe akiwa waziri wa mambo ya nje, shilingi bilioni 356.324 zilitumika kwa safari za nje huku tiketi za ndege peke yake zikigharimu bilioni 183.160. 

Taasisi zilizoongoza kwa matumizi hayo ni pamoja na wizara ya mambo ya nje aliyokuwa anaihudumia ndugu Membe. 

Tunajiuliza, ni trilioni ngapi zilitumika kwa safari za nje katika kipindi chote cha miaka 8 ambacho ndugu Membe alikuwa waziri? 

Je, huu haukua mzigo kwa taifa? Ndugu Membe anazungumziaje matumizi haya mabovu ambayo yalifanyika yeye akiwa na dhamana ya wizara hiyo?

Watanzania wote tunafahamu na kukubali kuwa safari hizi zilikua mzigo mkubwa kwa taifa, na tunaunga mkono juhudi za kupunguza na kudhibiti safari zisizo za lazima.

BERNARD MEMBE SI MKWELI
Ndugu waandishi, ili kudhihirisha kuwa ndugu Bernard Membe si mkweli kwa anayoyasema kuhusu safari za nje, na kwamba kauli zake kuhusu jambo hili zinakinzana, baada ya hotuba ya Rais Dr. John Magufuli bungeni mjini Dodoma, bwana Membe alinukuliwa akimpongeza mh Rais kwa uamuzi wake wa kupunguza safari za nje kwani kwa maneno yake alisema walikua wanapishana angani kama vile nyumbani kunawaka moto.

Ni Bernard Membe huyuhuyu ambaye leo anatafuna maneno yake bila aibu na kutueleza kuwa safari zile zilikua na neema kwa taifa.

KUHUSU KUTOKUA NA BALOZI KATIKA NCHI ZOTE
Katika kuhalalisha safari za nje zisizo za lazima, ndugu Membe alieleza kuwa Tanzania ina mabalozi 36 tu katika nchi 194 ambazo tunapaswa kuwa na mabalozi.

Tunapenda kumfahamisha ndugu Membe kuwa kutokuwa na balozi katika nchi zote sio kigezo cha kutumia mabilioni ya pesa kwa ajili ya safari zisizo na tija kwa taifa.

Kutokana na kuwa uchumi wetu bado unakua, na haustahamili gharama za kuweka mabalozi katika nchi zote, wako mabalozi wetu nje ya nchi ambao wanawakilisha nchi zaidi ya moja zilizoko katika ukanda mmoja. 

Mfano, balozi Ombeni Sefue aliwahi kuwa balozi wetu Marekani akiwakilisha pia CUBA. Aidha, uamuzi wa nchi kufungua ubalozi katika nchi nyingine hutegemea vigezo mbalimbali kama faida za kiuchumi, kisiasa, kiusalama na kidiplomasia.

RAISI HAJAKATAA KUSAFIRI NJE YA NCHI
Ndugu Membe anapotosha ukweli anaposema Tanzania sio kisiwa na kwamba Raisi na waziri wake wa mambo ya nje lazima wasafiri nje ya nchi watake wasitake.

Tunapenda kumfahamisha ndugu Membe kuwa, mh. Raisi Dr. John Magufuli hajatoa kauli kuwa yeye au wasaidizi wake hawatosafiri nje ya nchi katika safari  muhimu na zenye tija. Isipokuwa, muongozo wa mh. Rais kuhusu safari za nje unalenga kupunguza safari zile ambazo hazina ulazima na tija kwa taifa.

KUHUSU MGOGORO WA UCHAGUZI WA ZANZIBAR
Katika maelezo aliyonukuliwa na gazeti la Mwananchi, ndugu Membe alieleza kupinga kufutwa kwa matokeo yote ya uchaguzi wa Zanzibar yakiwemo ya wawakilishi, na kwamba jambo hili limeihuzunisha dunia.

Kauli hii ya ndugu Membe inatushangaza na kutusikitisha sana. Kwanza tunajiuliza, Je, ikiwa sehemu kubwa ya uchaguzi iligubikwa na udanganyifu na ukiukwaji wa taratibu za uchaguzi kinyume na sheria za uchaguzi wa Zanzibar, ni kwanini ndugu Membe ashangae uchaguzi wote kufutwa na tume ya uchaguzi ZEC?

Tunamtaka ndugu Membe atueleze, ni dunia ipi hiyo inayotushangaa?

Ni kwanini dunia hiyo anayoitetea ndugu Membe haijashangaa kumuona maalim Seif Shariff Hamad akijitangaza kuwa mshindi kinyume cha sheria za uchaguzi?

Ndugu Membe anapaswa kushangaa, ni kwanini hadi leo hii maalim Seif Shariff Hamad hajakamatwa na kufikishwa mahakamani kujibu mashitaka ya kujitangaza kuwa mshindi kinyume cha sheria.

KUHUSU VIKAO VYA MARIDHIANO
Kuhusu vikao vya maridhiano vilivyokua vinaendelea, ndugu Membe amekosoa kitendo cha Raisi wa Serikali ya mapinduzi ya Zanzibar na maalim Seif Shariff hamad kuachwa wakazungumza wenyewe wawili.

Kwanza tunasikitika kuwa ndugu Membe huenda ama hajui kinachoendelea Zanzibar au ameamua kupotosha umma kwa makusudi.

 Hii ni kwasababu mazungumzo yaliyokua yakiendelea Zanzibar, hayakuwahusisha Dr. Shein na maalim Seif Shariff peke yao. 

Bali yalishirikisha marais wastaafu wa Zanzibar, Raisi wa serikali ya mapinduzi ya Zanzibar, Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar na makamu wa pili wa Rais wa Zanzibar.

Pili, katika muafaka wa kisiasa wa Zanzibar wa mwaka 2009/2010 uliopelekea kuundwa kwa serikali ya umoja wa kitaifa, kwa kiasi kikubwa ni maalim Seif Shariff hamad na Rais wa Zanzibar wa wakati huo mh. Amani Abeid Karume pekee walioshiriki mazungumzo.

RAI KWA NDUGU MEMBE
Mosi, tunapenda kumkumbusha ndugu Bernard Membe kuwa yeye ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM taifa amewahi kuwa mjumbe wa kamati kuu ya CCM. 

Hivyo anajua utaratibu wa Chama na anayo nafasi ya kuyasema mawazo yake juu ya uendeshaji wa serikali ndani ya vikao halali vya chama. 

Aidha, ndugu Membe kwa nafasi yake kama mjumbe wa NEC na waziri wa zamaniwa mambo ya nje na ushirikiano wa kimataifa, anayo nafasi ya kutoa ushauri na maoni yake moja kwa moja kwa Raisi wa jamhuri ya muungano wa Tanzania mh. Dr. John Magufuli, Mwenyekiti wa CCM taifa Dr. Jakaya Kikwete au kwa Katibu Mkuu wa CCM ndugu Abdulrahman Kinana.

Kutotumia fursa hizo kutoa maoni yake ni kujishushia heshima mbele ya jamii.

Pili, tunamkumbusha ndugu Membe kuwa yeye sasa ni mstaafu aliyeitumikia nchi yake kwa muda mrefu na nafasi mbalimbali. 

Ni vema sasa akatoa fursa kwa viongozi wengine walioko madarakani kutimiza wajibu wao wa kuwatumikia watanzania. Muda wake umekwisha na sasa ni busara akakaa kimya na kuchunga maneno yake.

Raisi mstaafu wa awamu ya tatu mh. Benjamin William Mkapa aliwahi kusema (nanukuu):-

"Siku moja mtoto mdogo aliwahi kuniuliza. Nani ni bingwa wa kuendesha shughuli za serikali? Nikatafakari sana swali lile, kisha baada ya muda nikamjibu…Ni mwanasiasa aliyestaafu kisha akachunga ulimi wake…"

MWISHO
Tunamshauri ndugu Membe kuuchukua ushauri huu wa Raisi mstaafu Benjamin Mkapa, utamsaidia. Aidha tunamtaka afahamu kwamba watanzania wana imani kubwa na juhudi zinazofanywa na serikali katika kupunguza matumizi, kuziba mianya ya rushwa, ukwepaji kodi na ubadhirifu wa mali za umma. 

Wakati huu si wa kupika majungu, fitina wala ubabaishaji. Ni wakati wa kuungana pamoja kama taifa na kuchapa kazi tu.

Asanteni.

Imetolewa na ndugu

ALLY S. HAPI
KATIBU WA IDARA,
ELIMU, UTAFITI NA UONGOZI,
SHIRIKISHO LA VYUO VYA ELIMU YA JUU TANZANIA

No comments: