Tanzania Hatarini Kukubwa Na Mafuriko Ya El-nino - Umoja Wa Mataifa - LEKULE

Breaking

16 Jan 2016

Tanzania Hatarini Kukubwa Na Mafuriko Ya El-nino - Umoja Wa Mataifa


UMOJA wa Mataifa umeihadharisha Tanzania kuwa itakumbwa na mafuriko yatakayosababishwa na mvua za El-Nino na kutaka kuanza kuchukua tahadhari mapema.

Taarifa ya Umoja huo ya uwezekano mkubwa wa mafuriko yatakayosababishwa na mvua za El- Nino imetolewa wakati serikali inaendelea kubomoa nyumba zilizojengwa maeneo hatarishi katika mabonde na maeneo yasiyoruhusiwa.

Kwa mujibu wa taarifa ya Katibu Mkuu Msaidizi Mwandamizi anayehusika na Misaada ya Kibinadamu na Uratibu wa Misaada ya Dharura, Stephen O’Brien, Tanzania inaweza kukabiliwa na mafuriko ya El-Nino kati ya mwezi huu wa Januari na Machi, mwaka huu.

Pamoja na Tanzania, nchi nyingine ambazo zimetajwa kukumbwa na mafuriko hayo makubwa ni pamoja na Madagascar, Malawi na Msumbiji. 
Taarifa ya O’Brien kuhusu madhara ya El-Nino na namna gani Jumuiya ya Kimataifa inatakiwa kujiandaa au inajiandaa na kadhia hiyo iliwasilishwa mbele ya wajumbe wa nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa na nakala yake kutumwa kwa Uwakilishi wa Kudumu wa Tanzania katika Umoja wa Mataifa.

Pamoja na kutoa tahadhari hiyo, O’Brien amezisihi nchi ambazo zinatarajiwa kukumbwa na maafa ya El -Nino kujiandaa ipasavyo na kuyataja maandalizi hayo kuwa ni pamoja na utoaji wa misaada ya kibinadamu kwa wananchi watarajiwa wa athari za mvua hizo.

Kwa mujibu wa Katibu Mkuu Msaidizi Mwandamizi, upande wa Afrika ya Mashariki, nchi kadhaa hususan ukanda wa magharibi zimekumbwa na uhaba mkubwa wa mvua na hivyo kuathiri kiwango cha upatikanaji wa chakula.

Nchi hizo ni Ethiopia, Sudan, Djibouti na Eritrea ilihali baadhi ya nchi zikipata kiwango cha mvua kilichovuka mipaka. “ Kuanzia mwezi Januari hadi Machi, nchi za Tanzania, Msumbiji, Madagascar na Malawi zina uwezekano mkubwa wa ku kumbwa na mafuriko ya El- Nino,” alisema O’Brien.

Alisema nchi hizo zitahitaji pamoja na mambo mengine misaada ya kujiandaa na kushughulikia kile kinachotabiriwa kwani kina uwezekano mkubwa wa kutokea.
Ukiacha nchi za Afrika ya Mashariki, nchi nyingine kwa upande wa Afrika ambazo zimekumbwa na hali tete ya uhaba wa mvua na hivyo kutishia usalama na upatikanaji wa chakula ni Angola, Botswana, Malawi, Namibia, Afrika Kusini, Swaziland, Zambia na Zimbabwe.

O’Brien alisema nchi hizo zimekuwa na uhaba wa mvua kiasi kwamba zitakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula na kusababisha watu zaidi ya milioni 28 katika mataifa hayo kukukosa chakula.

Akizungumzia kuhusu misaada ambayo imekwishakutolewa na nchi wahisani ili kukabilia na ukame na madhara yatokanayo na El-Nino , Katibu Mkuu Msaidizi Mwandamizi huyo alisema kuwa hadi wakati anatoa taarifa yake kiasi cha Dola za Marekani milioni 360 kilikuwa kimetolewa na wafadhili kwa lengo la kukabiliana na madhara yatakayotokana na ElNino ikiwa ni pamoja na usalama wa chakula.

Pamoja na michango hiyo, O’Brien alisema haitoshi kutokana na ukweli kwamba maafa yatakayotoka na madhila ya El-Nino yanahitaji misaada zaidi.
Mbali ya nchi za kanda ya Afrika baadhi ya nchi nyingine ambazo zitakumbwa na zilishawahi kupata balaa la El-Nino ni pamoja na nchi ambao zimo katika Bara la Latini Amerika na nchi za eneo la Pasifiki ambazo nyingi ni visiwa.

Shirika la Kimataifa la Hali ya Hewa (WMO) linatarajiwa Mwezi Februari kutoa taarifa zaidi kuhusu mwelekeo za mvua hizo za El-Nino. 
Mvua kama hizo zilishawahi kunyesha nchini Tanzania mwaka 1998 na kusababisha maafa makubwa na watu kadhaa walipoteza maisha, huku maelfu wengine wakijeruhiwa na kupoteza makazi.


Mwaka jana mwezi Agosti Mamlaka ya Hali ya Hewa Tanzania (TMA) ilitoa tahadhari kuwa Tanzania ni kati ya nchi za Barani Afrika zitakazokumbwa na mvua za El Nino kati ya mwezi Septemba na Desemba, mwaka jana.

No comments: