TANESCO Yakanusha Kuuza Asilimia 49 ya Hisa Zake - LEKULE

Breaking

7 Jan 2016

TANESCO Yakanusha Kuuza Asilimia 49 ya Hisa Zake

Tunakanusha taarifa iliyochapishwa na gazeti la The Citizen la Januari 5, 2016 katika ukurasa wake wa 12 yenye kichwa cha habari: ‘Umma kununua asilimia 49 ya hisa za Tanesco’. Mwandishi na Mhariri wamejiandikia taarifa hiyo kwa sababu wanazozijua wao.

Sehemu ya taarifa inasema: Serikali ya Tanzania ina mpango wa kuuza hisa ya Shirika la Umeme Tanzania kwa umma...

Pia, sehemu nyingine inasema: Waziri wa Nishati na Madini Sospeter Muhongo aliliambia gazeti la East African kuwa Serikali itatoa asilimia 49 ya hisa za Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) wakati huo Serikali ikibaki na hisa zingine...

Tungependa wananchi kwa ujumla waelewe kwamba taarifa hiyo si sahihi na inapotosha umma. Taarifa sahihi kama ifuatavyo:
  • Kwanza, Waziri Sospeter Muhongo hajafanya mahojiano yoyote na mwandishi wa gazeti hilo la The East African wala gazeti la The Citizen. 
  • Pili, Serikali haina mpango wa kuuza hisa za TANESCO kwa umma.
Mkakati uliopo wa Mageuzi ya kuboresha Shirika la Umeme Tanzania (TANESCO) ujulikanao kama Electricity Supply Industry Reform Strategy and Roadmap (ESI-RSR) 2014 – 2025 ni kama ifuatavyo:

MAELEZO YA MKAKATI NA MWELEKEO WA KUREKEBISHA SEKTA NDOGO YA UMEME (ESI-RSR)
Mwezi Juni 2014, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilipitisha na kuchapisha mkakati wa mageuzi wa Electricity Supply Industry Reform Strategy and Roadmap (ESI-RSR) 2014 – 2025.

Lengo la msingi wa mkakati huo ni kuboresha mazingira ya uwekezaji wa sekta binafsi katika nyanja za uzalishaji na usambazaji, na kuongeza uunganishaji wa umeme katika ngazi zote.

Utekelezaji wa mpango huo ambao unatarajiwa kutekelezwa katika kipindi cha miaka kumi na moja (11) umegawanyika katika vipindi vikuu vitatu ambavyo ni muda mfupi, wa kati na muda mrefu.

=>Mkakati wa muda mfupi ni kutenganisha shughuli za Uzalishaji ili zifanywe na Kampuni Tanzu ya TANESCO.

Umiliki wa uzalishaji, usafirishaji na usambazaji chini ya awamu hii itaendelea kuwa chini ya Serikali, kama mbia moja.

=> Mkakati wa muda wa kati unahusu kutenganisha sehemu ya usambazaji kutoka kwenye usafirishaji. Katika Awamu hii,Kampuni za uzalishaji, usafirishaji na usambazaji zitaendelea kuwa chini ya umiliki wa Serikali.

=>Mkakati wa muda mrefu utahusishaOfisi za Kanda kujihusisha na usambazaji wa huduma za umeme ambazo pia zitagawanywa kulingana na uwezo wa kujiendesha. 
Katika kipindi hicho cha muda mrefu, kampuni binafsi za usambazaji umeme zitaendelea kushiriki katika shughuli za uzalishaji na usambazaji umeme kwa ajili ya kuchochea ushindani na ufanisi kwenye soko.

Tunawahimiza wadau wote kusoma mkakati wa mageuzi ujulikanao kama Electricity Supply Industry Reform Strategy and Roadmap (ESI-RSR) 2014 – 2025 ambao unapatikana mitandaoni
 
Aidha, tunawakumbusha Waandishi wa Habari na Wahariri ambao hawazingatii maadili ya taaluma yao kuandika taarifa sahihi ili kuepusha upotoshaji kwa umma.

Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano Serikalini

6 Juni, 2015

No comments: